Ujumbe wa Baba Mtakatifu katika Kesha la kufunga Siku ya 28 ya Vijana Duniani, Rio
2013
Kesha la Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013 limefanyika kwenye
Ufuko wa Copacabana, Rio de Janeiro, Brazil na kuhudhuriwa na bahari ya vijana kutoka
sehemu mbali mbali za dunia. Kesha hili liligawanyika katika sehemu kuu mbili, yaani
Liturujia ya Neno la Mungu na Ibada ya Kuabudu Ekaristi Takatifu. Vijana wamefanya
onesho linaloangalisha umuhimu wa vijana kushiriki katika ujenzi wa Kanisa la Kristo.
Wahusika wakuu katika sehemu hii, walikuwa ni vijana Wafranciskani.
Vijana
wametoa ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa lake na baadaye wakamuuliza Baba
Mtakatifu Francisko maswali kadhaa. Baba Mtakatifu anasema, Mtakatifu Francisko wa
Assis alipokuwa kwenye tafakari ya kina, alisikia sauti ya Kristo ikimwalika kumjengea
Kanisa, yaani kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa kwa njia ya huduma
makini. Hata leo hii, Kristo anahitaji vijana wachangamfu na wenye imani thabiti wanaoweza
kujitosa kimaso maso kwa ajili ya kutangaza na kumshuhudia Kristo sehemu mbali mbali
za dunia kwa njia ya maisha yao adili.
Baba Mtakatifu anasema, Mwenyezi Mungu
anaendelea kupandikiza mbegu ya Neno lake katika moyo wa kila kijana, changamoto na
mwaliko kwa kila kijana kutoa nafasi ili Neno la Mungu liweze kupata maskani katika
moyo na maisha ya kijana. Neno hili likue na kukomaa, kwa kutambua kwamba, wao ni
Wakristo "Full Time" na wala si Wakristo wa kipindi cha mpito, kama moto wa mabua!
Ni Wakristo wa kweli na wema mbele ya Mwenyezi Mungu; wanaoishi katika uhuru wao bila
ya kumezwa na malimwengu, kwa kutambua kwamba, Yesu Kristo ni njia, ukweli na uzima.
Baba Mtakatifu anawaambia vijana kwamba, Yesu Kristo anawaalika kuacha yote
na kumfuasa maisha yao yote ili waweze kutenda kama Jumuiya, jambo ambalo linahitaji
mazoezi. Hii ndiyo changamoto pia iliyoko mbele ya wafuasi wa Kristo wanaopaswa kufanya
mazoezi ili kuwa na maisha bora, yanayozaa matunda ya utakatifu wa maisha, ili hatimaye,
waweze kupata maisha ya uzima wa milele.
Ili kufanikisha changamoto hii,
kuna haja ya kujenga na kuimarisha majadiliano ya kina na Yesu Kristo kwa njia ya:
Sala ambayo ni majadiliano ya kila siku na Mwenyezi Mungu kwa kutambua kwamba, Mwenyezi
Mungu, daima anawasikiliza; Ushiriki mkamilifu wa Sakramenti unawawezesha kuonja uwepo
wa Mungu kadiri ya mapenzi ya Yesu; kwa njia ya upendo wa kidugu, wataweza kusikilizana,
kufahamiana, kusameheana, kupokeana na kusaidiana bila kuwatenga wala kuwasukumiza
wengine pembezoni.
Baba Mtakatifu anawakumbusha vijana kwamba, mioyo yao ni
udongo mzuri ambao unaweza kupokea Neno la Mungu, hata pale wanapopambana kulimwilisha
Neno hili katika uhalisia wa maisha yao, watambue kwamba, wao ni sehemu ya Familia
inayofanya hija hii ya maisha; wao ni sehemu ya Kanisa na kwamba, wanachangamotishwa
kuwa ni wadau na wajenzi wa Kanisa na historia kwa ujumla. Vijana ni mawe hai katika
ujenzi wa Kanisa hai la Yesu linaloweza kuwakumbatia watu wote. Kanisa halina budi
kuwa ni kwa wote.
Baba Mtakatifu Francisko anahitimisha tafakari yake katika
Kesha la Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa kuwakumbusha kwamba, Yesu bado anamwambia
kila mmoja wao, kwamba, "Basi enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa ni wanafunzi."
Mama Teheresa wa Calcutta anasema, mchakato huu wa mabadiliko ndani ya Kanisa unaanza
kwako na kwangu pia!