Padre Federico Lombardi, Msemaji mkuu wa Vatican anabainisha kwamba, Baba Mtakatifu
Francisko siku ya Ijumaa asubuhi kwenye kitongoji cha Quinta de Boa amewaungamisha
vijana watano kwenye hema lililokuwa limeandaliwa kwa ajili ya maungamo kwa vijana.
Watawa wa Shirika la Wamissionari wa Upendo, maarufu kama Watawa wa Mama Theresa
wa Calcutta, waliwasindikiza vijana waliokuwa wanaungama kwa Ibada ya Kuabudu Ekaristi
Takatifu. Hawa ni vijana waliochaguliwa kwa bahati nasibu. Baba Mtakatifu alisali
kwa ukimya na baadaye akaanza kuungamisha kadiri ya Mapokeo ya Kanisa. Ametumia dakika
25 kuwaonjesha vijana hawa huruma na upendo wa Mungu katika maisha yao kwa njia ya
Sakramenti ya Upatanisho. Vijana wengi wametumia siku hii kwa ajili ya kujipatanisha
na Mungu pamoja na jirani zao.
Baba Mtakatifu Ijumaa mchana alipata pia fursa
ya kuzungumza na vijana sita waliokuwa wanatumikia kifungo gerezani. Amezungumza pia
na viongozi wa Kanisa na Gereza waliokuwa wamewasindikiza vijana hawa. Viongozi wa
gereza wamemshukuru Baba Mtakatifu na Kanisa kwa ujumla kutokana na huduma makini
wanayotoa kwa ajili ya wafungwa magerezani: kiroho na kimwili.
Vijana hao
wamemshirikisha Baba Mtakatifu Francisko hali na magumu wanayokabiliana nayo gerezani;
wamempatia barua kutoka kwa wafungwa kwa niaba ya wafungwa wenzao. Kimsingi wamemshukuru
na kuahidi kuendelea kumwombea Baba Mtakatifu katika maisha na utume wake. Wamemzawadia
Baba Mtakatifu Rozari waliyoitengeneza wakiwa gerezani, huku wakionesha majina ya
vijana waliouwawa kikatili nchini Brazil, takribani miaka 20 iliyopita.
Baba
Mtakatifu amesema hakuna haja ya kufanya vurugu, bali kumwilisha upendo. Kwa pamoja
waliweza kusali kwa ajili ya kuwaombea vijana hao na Baba Mtakatifu amewaalika waendelee
kusali pia kwa ajili ya maisha na utume wake. Padre Federico Lombardi anasema huu
ndio mwelekeo wa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani, si tu kwa wale wanaobahatika
kufika, bali vijana wote walioenea sehemu mbali mbali za dunia, katika raha, shida
na mahangaiko yao ya ndani.
Baba Mtakatifu Francisko wakati wa chakula cha
mchana, aliwaona vijana wakiwa na wasi wasi, akawauliza mbona mna wasi wasi hivi,
wao wakasema, kwa mara ya kwanza katika maisha ya ujana wao wamebahatika kula pamoja
na Baba Mtakatifu. Baba Mtakatifu amezungumza na vijana hawa akiwauliza kuhusu dira
na mwelekeo wa dhana ya Kanisa waliyo nayo moyoni mwao na kwamba, amewataka kamwe
wasikate wala kukatishwa tamaa, wajitahidi kuishi katika Jumuiya na kamwe wasigubikwe
na ubinafsi, waoneshe dunia inayosimikwa katika utu na maisha ya binadamu!
Tatizo
kubwa katika ulimwengu mamboleo ni vijana kugeuzwa kuwa ni vichokoo na vivutio vya
masuala ya uchumi. Amewataka vijana kuhakikisha kwamba, wanajitahidi kuboresha maisha
yao ya kiroho, pale inapowezekana kuwa na Mlezi wa maisha ya kiroho, anayeweza kumsindikiza
katika safari yake ya ndani, huku wakiendelea kuwaonjesha wengine upendo unaobubujika
kutoka kwa Mwenyezi Mungu, aliyewapenda upeo.
Baba Mtakatifu anawataka vijana
hao kujiuliza swali la msingi juu ya uwepo wao kwenye Maadhimisho ya Siku ya Vijana
Duniani; Kwa nini kuna mateso na mahangaiko mengi duniani? Mbona watu wanaendelea
kupoteza maisha yao kutokana na baa la njaa wakati dunia inaweza kuzalisha chakula
cha kutosha kwa watu wengi zaidi?
Baada ya sala, Baba Mtakatifu amewapatia
zawadi kama kumbu kumbu ya mlo wao wa pamoja! Vijana wanasema, kamwe, hawataweza kusahau
tukio hili katika maisha yao! Kujichana na Baba Mtakatifu, kwa hakika si haba!