2013-07-27 07:21:04

Familia ni mahali muafaka pa kurithisha imani, matumaini na mapendo!


Baba Mtakatifu Francisko, Ijumaa tarehe 26 Julai 2013 ameianza siku kwa Ibada ya Misa takatifu, baadaye akajiunga na Makleri wengine waliokuwa wanaungamisha vijana, tayari kujipatia rehema na neema zinazotolewa na Mama Kanisa katika Maadhimisho haya. Baba Mtakatifu akiwa kwenye Makao makuu ya Jimbo kuu la Rio de Janeiro amekutana na kuzungumza na baadhi ya vijana wanaotumikia vifungo kwenye magereza ya Rio de Janeiro.

Baba Mtakatifu Francisko wakati wa mlo wa mchana amejumuika na vijana kumi na wawili ambao ni wawakilishi wa vijana kutoka mabara matano na vijana wawili kutoka Brazil wamepata nafasi ya upendeleo kwa kuwa ni wenyeji wa Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013.

Wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana, Kumbu kumbu ya Watakatifu Joakim na Anna, wazazi wake Bikira Maria, Baba Mtakatifu akiwa kwenye Makao makuu ya Jimbo kuu la Rio de Janeiro amewashukuru waamini kwa mapokezi na ukarimu mkubwa waliomwonesha kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Ni matumaini ya Baba Mtakatifu Francisko kwamba, uwepo wake mjini Rio utaamsha ari, moyo na upendo kwa Kristo na Kanisa lake; wakionesha furaha ya kuungana na kuwa ni sehemu ya Kanisa, sanjari na kutambua wajibu na dhamana ya kuishi na kushuhudia imani.

Baba Mtakatifu anasema katika Familia ya Watakatifu Joakim na Anna, Bikira Maria alijifunza kusikiliza na hatimaye, kumwilisha mapenzi ya Mungu katika hija ya maisha yake. Watakatifu hawa wamechangia kwa kiasi kikubwa mnyororo uliowaonjesha upendo wa Mungu mintarafu dhamana ya familia hadi kufikia kwa Bikira Maria, aliyempokea Neno wa Mungu na kumtoa kama zawadi kubwa kwa ulimwengu. Tukio hili linaonesha umuhimu wa Familia kama sehemu maalum kwa ajili ya kurithisha imani.

Baba Mtakatifu Francisko amekumbusha kwamba, nchini Brazil na Amerika ya Kusini kwa ujumla, Siku kuu ya Watakatifu Joakim na Anna ni Siku kuu ya Mabibi na Mababu. Kundi hili ni muhimu sana katika Jamii kwani wana dhamana ya kurithisha tunu msingi za maisha ya kiimani, kiutu na kijamii kwa Jamii inayowazunguka. Kumbe, kuna haja kwa vijana wa kizazi kipya kukutana na kudumisha majadiliano kati yao na wazee hususan ndani ya familia.

Baba Mtakatifu Francisko anahitimisha tafakari yake wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana kwa kukumbusha kwamba, watoto na wazee ni hazina ya jamii; watoto kwa wakati muafaka, watabeba historia ya Jamii zao na wazee wana jukumu la kurithisha uzoefu na mang'amuzi ya maisha.

Vijana wanaohudhuria Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani wanapenda kuwasalimia Bibi na Babu zao, waliotawanyika sehemu mbali mbali za dunia. Baba Mtakatifu anawashukuru na kuwapongeza kwa ushuhuda na hekima wanayoendelea kutoa kwa vijana wa kizazi kipya hadi sasa.







All the contents on this site are copyrighted ©.