Vijana wameitikia wito na ukarimu wa Yesu, wanataka kujenga na kuimarisha imani na
urafiki wao kwa Kristo!
Baba Mtakatifu Francisko Alhamisi jioni, tarehe 25 Julai 2013 kama sehemu ya Maadhimisho
ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani aliupokea rasmi umati wa vijana kutoka sehemu mbali
mbali za dunia wanaoshiriki katika Maadhimisho ya Siku ya Vijana huko Rio de Janeiro.
Tukio hili lilifunguliwa kwa onesho la sanaa ambalo, vijana walionesha hali halisi
ya maisha yao ya kila siku, baadaye ilifuata Liturujia ya Neno la Mungu, wakiongozwa
na kauli mbiu "Bwana ni vizuri sisi kuwapo hapa".
Baba Mtakatifu katika tafakari
yake amewaambia vijana kwamba, ana matumaini makubwa na vijana na anawatakia hija
njema katika maisha yao ya ujana, daima wakiwa waaminifu kwa Kristo huku wakiendelea
kukumbatia Fumbo la Msalaba. Baba Mtakatifu amewakumbuka vijana waliopoteza maisha
na kujeruhiwa wakati wakiwa njiani kwenda Rio de Janeiro kwa ajili ya Maadhimisho
ya Siku ya Vijana Duniani.
Amewashukuru vijana kwa kuitikia wito kutoka kwa
Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, ili kuja kuadhimisha siku kuu ya
imani. Ni umati mkubwa wa vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia, ukiwa na mila,
desturi na tamaduni zao, lakini wote kwa pamoja wanaunganishwa na imani na hamu ya
kutaka kukutana na Yesu, ili waweze kuwa ni wanafunzi wake. Kwa juma zima, mji wa
Rio umekuwa ni kiini cha maisha na utume wa Kanisa, hali inayoonesha jinsi ambavyo
vijana wameitikia kwa ukarimu na ujasiri wito wa Yesu na wanaendelea kubaki pamoja
naye ili wajenge urafiki wa kudumu.
Baba Mtakatifu anawaambia vijana waliokuwa
wamekusanyika kwenye ufuko wa Copacabana kwamba, hata leo hii, Yesu anamwita kila
mmoja wao kuwa ni mfuasi na rafiki yake mwaminifu, ili aweze kuwa ni shahidi wa Injili.
Hii ni changamoto pevu kwa kila mwamini hasa wakati huu wa Maadhimisho ya Mwaka wa
Imani. Vijana wamepata urithi mkubwa wa zawadi ya imani kutoka katika familia na jumuiya
zao za Kikristo. Uwepo wake nchini Brazil unapania kuwaimarisha katika imani na ari
ya kuwa ni wafuasi wa Kristo.
Baba Mtakatifu ametumia fursa hii kuwasalimia
na kuwatakia kheri na baraka vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia, wanaposhiriki
katika Siku kuu ya Imani; wakiwa wameungana kwa pamoja, hali inayoonesha urafiki na
imani pamoja na kutambua kwamba, wote hawa anapenda kuwakumbatia kama Mchungaji mkuu
wa Kanisa, huku wakipokelewa na kubarikiwa na Yesu Kristo Mfalme.
Baba Mtakatifu
amewashukuru na kuwapongeza wadau mbali mbali waliojitaabisha ili kuhakikisha kwamba,
Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani yanapata mafanikio makubwa. Haya ni maandalizi
yaliyotekelezwa tangu vijana walipokuwa Majimboni mwao. Anawashukuru wakuu wa Serikali
na Kanisa waliochangia kwa hali na mali katika kufanikisha Maadhimisho haya ambayo
ni kielelezo cha umoja, imani na udugu. Na kwa maneno haya, Baba Mtakatifu Francissko
alikuwa anafungua rasmi Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013.
Katika hotuba yake, Askofu mkuu Oran Joao Tempesta wa Jimbo kuu la Rio,
amemshukuru Baba Mtakatifu Francisko na bahari ya vijana iliyokuwa imekusanyika kwenye
ufuko wa Copacabana kuadhimisha Mafumbo ya Imani, huku wakionesha furaha ya ujana
wao na ushuhuda wao kwa Kristo na Kanisa lake. Ni tukio ambalo linafuatiliwa na umati
mkubwa wa vijana kwa njia ya vyombo vya upashanaji habari, kwa sala na sadaka yao.
Uwepo wa Baba Mtakatifu ni kielelezo cha umoja wa kimissionari unaoimarisha
hija ya pamoja inayofanywa na wafuasi wa Kristo wanaoandamana kwenda nyumbani kwa
Baba. Hiki ni kipindi ambacho vijana wengi wamegundua na kuonja fadhila ya matumaini
ndani mwao.
Vijana kutoka katika nchi 180 wamewakilishwa, kama kielelezo cha
ndoto ya vijana duniani. Kuna umati mkubwa wa vijana ambao umekata tamaa kutokana
na kumezwa mno na malimwengu, ubinafsi, ukosefu wa haki na usawa katika Jamii na wakati
mwingine wamejikuta wakitumbukia katika furaha ya muda ambayo imegeuka kuwa ni kilio!
Askofu
mkuu Tempesta anasema vijana wanazungukwa na upendo wa Mungu katika hija ya maisha
yao, kwa njia ya imani wanapenda kukabiliana na changamoto za maisha, ili Kristo aweze
kufahamika na kupendwa zaidi katika medani mbali mbali za maisha; kila kijana katika
hija yake aungame imani inayomwilishwa katika utume.
Wawakilishi wa Vijana
kutoka katika Mabara matano, wamemkaribisha Baba Mtakatifu Francisko, ndani mwao wakiwa
wamewabeba na kuwakumbatia ndugu zao katika imani, waliomwilisha Injili na wanaoendelea
kuitolea ushuhuda sehemu mbali mbali za dunia. Kwa vijana kutoka Asia, wanasema, wanawakumbatia
ndugu zao katika Kristo ambao wameendelea kutangaza Injili na kuishuhudia kwa njia
ya majadiliano ya kidini na kiekumene.
Mwakilishi wa vijana kutoka Barani
Afrika anasema, vijana wanapenda kumkaribisha kwa moyo mkunjufu huku wakisukumwa na
ari na moyo wa kimissionari, licha ya magumu na changamoto nyingi wanazokabiliana
nazo. Vijana kutoka Oceania wanasema, umbali si kikwazo kwa wafuasi wa Kristo katika
mchakato wa kudumisha umoja na udugu, kwani wanatambua kwamba, wote ni ndugu katika
Kristo.
Vijana kutoka Amerika na kwa namna ya pekee wale wa Brazil wamemwambia
Baba Mtakatifu kwamba, inapendeza wao kukaa pamoja. Hii ni zawadi kubwa ambayo wangependa
kumkirimia, huku wakimwonesha furaha, umoja na sala zao.