2013-07-25 08:01:38

Biashara na matumizi haramu ya dawa za kulevya ni janga kubwa miongoni mwa vijana!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumatano jioni tarehe 24 Julai 2013 alitembelea na kufungua Hospitali ya Mtakatifu Francisko wa Assisi inayowahudumia wagonjwa wa akili, madhabahu ya mahangaiko na mateso ya mwanadamu; kielelezo cha toba na wongofu wa ndani uliofanywa na Mtakatifu Francisko wa Assisi unaoendelezwa na wafuasi wake hadi leo hii kwa kuwamegea wagonjwa furaha na matumaini, lakini zaidi kwa njia ya huduma makini.

Wanatambua kwamba, kila sura ya mgonjwa inamwonesha Yesu Mteswa. Baba Mtakatifu anasema, uwepo wake mahali hapo ni kutaka kuonesha mshikamano wa upendo unaotolewa na Mama Kanisa, ili waonje matumaini katika hija ya maisha yao ya kila siku!

Baba Mtakatifu anawaalika watu kujifunza kukumbatia kwani kuna hali nchini Brazil na sehemu mbali mbali za dunia zinazohitaji kupewa kipaumbele cha pekee badala ya kuendelea kukumbatia utamaduni wa kifo, unaofumbatwa katika uchu wa mali na madaraka kwa gharama kubwa.

Tatizo la biashara na matumizi haramu ya dawa za kulevya ni janga kubwa Amerika ya Kusini, changamoto ya kupambana fika na janga hili kwa kujikita katika ujenzi wa misingi ya haki; kwa kuwaelimisha vijana maana na tunu msingi za maisha ya pamoja, sanjari na kuendelea kuwasaidia walioathirika na matumizi haramu ya dawa za kulevya. Huduma hii ifanywe kwa upendo wa Kristo, kwa kujifunza kuwakumbatia wenye shida na mahangaiko, kwa kuwaonesha ukaribu, huruma na upendo.

Baba Mtakatifu anawahimiza waamini na watu wenye mapenzi mema, kuwasaidia kwa hali na mali wale waliotumbukia katika matumizi haramu ya dawa za kulevya, ili waweze kuwa na ujasiri wa kusimama tena, wakionesha nia na utashi wa kufanya hivyo. Kila mtu anawajibika katika maisha yake, jambo la msingi ni kuwa na ujasiri wa kutenda na hapo mtu anaweza kupata msaada.

Vijana katika hali kama hii, kamwe wasijisikie pweke, kwani Kanisa na watu wenye mapenzi mema, wanaendelea kufanya hija pamoja nao katika shida na mahangaiko yao ya ndani; wao wanapaswa kuwa ni watu wenye matumaini na kamwe, wasiache tumaini hili kuporwa na wajanja wachache. Kila mwamini awe ni chombo cha matumaini kwa jirani yake.

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuwa ni Wasamaria wema kwa jirani zao; watu wanaoguswa na shida na mahangaiko ya watu, kiasi hata cha kujitaabisha kuwahudumia. Hospitali ya Mtakatifu Francisko wa Assis ni kielelezo cha huduma ya Msamaria mwema, inayomjali mtu katika mahangaiko yake, ili hatimaye, aweze kuonja upendo. Chama cha Mtakatifu Francisko na wadau mbali mbali wanaotoa huduma kwa waathirika wa dawa za kulevya ni kielelezo cha watu wanaojitaabisha kuuona uso wa Kristo anayeteseka. Baba Mtakatifu Francisko amewashukuru wote kwa moyo wa dhati kabisa! Hii ni huduma wanayoitekeleza kwa ndugu zake Kristo.

Mwishoni, Baba Mtakatifu anawaalika wote kusimama kidete kupinga matumizi haramu ya dawa za kulevya; daima Kanisa litaendelea kuwasaidia katika shida na mahangaiko yao na kwamba, Kristo awe ni faraja na tumaini la maisha yao. Bikira Maria ataendelea kuwasaidia kubeba Msalaba kwa imani na matumaini.








All the contents on this site are copyrighted ©.