2013-07-23 11:10:40

Vijana angalieni kwa umakini madhara ya utandawazi, maendeleo ya sayansi na teknolojia!


Ndugu Francis Kilenga kutoka Dar es Salaam katika mahojiano na Radio Vatican anasema, dunia ni tambara bovu na ni sawa na mti mkavu! Vijana wanapaswa kuwa makini katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia, kamwe wasipende kujiingiza katika mambo ambayo yanaweza kuwapeleka pabaya! RealAudioMP3

Athari za utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia zimekuwa ni chanzo kikuu cha kumong'onyoka kwa misingi bora ya maadili na utu wema! Vijana wengi wanapenda kufuata na kuiga mkumbo wa yale wanayoyaona kwenye mitandao ya kijamii, matokeo yake ni kukosa dira na mwelekeo katika maisha.

Ndugu Francis Kilenga vijana wawe makini kwa mila na desturi njema za Kiafrika na Kitanzania, wawe na msimamo thabiti katika maisha ya kiroho na kimaadili, kamwe wasikubali kuyumbishwa kinyume cha utashi na msimamo wao wa maisha adili na manyofu. Vijana wamebarikiwa kuwa na karama na vipaji mbali mbali ambavyo vinapaswa kutumiwa kwa ajili ya ujenzi wa Kanisa, Familia na Jamii katika ujumla wake.

Ndugu Francis Kilenga, akizungumzia kuhusu Familia anasema, anapenda kuzihamasisha familia kufanya kazi kwa juhudi, bidii na maarifa kama sehemu ya mchakato wa kukamilisha utu na heshima yao kama binadamu. Ikumbukwe kwamba, kazi ni msingi wa maisha na uhai wa mwanadamu. Kazi itekelezwe kwa nidhamu na uaminifu mkubwa na kwa njia hii waamini wanaweza kutolea ushuhuda amini na mwenye mashiko kwa wale wanaowazunguka.

Hii ndiyo changamoto ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani na kwa namna ya pekee, wakati huu vijana wanapoadhimisha Siku ya Vijana Kimataifa huko Rio de Janeiro, Brazil.







All the contents on this site are copyrighted ©.