Rais wa Serikali ya Mpito ya Madagascar, Andry Rajoelina amewasili nchini kwa ziara
ya kikazi nchini Tanzania ambako baadaye atakuwa na mazungumzo na mwenyeji wake, Rais
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete.
Kwenye Uwanja wa Ndege
wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar Es Salaam, Rajoelina amepokelewa na mwenyeji wake,
Rais Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa Asasi ya Siasa, Ulinzi na Usalama (SADC-Troika)
ya Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC).
Katika nafasi yake ya
Mwenyekiti wa Asasi hiyo, Rais Kikwete ndiye amepewa jukumu na viongozi wenzake wa
nchi wanachama wa SADC kutafuta suluhisho la mgogoro wa kisiasa katika Kisiwa cha
Madagascar.
Viongozi hao wawili wamekutana Ikulu, Dar es Salaam ili kuzungumzia
hali ya kisiasa nchini Madagascar ambako Rais Kikwete atamweleza Rajoelina kuhusu
matokeo ya kikao cha wakuu wa nchi wanachama wa Asasi (SADC-Troika-Summit) kilichofanyika
chini ya uenyekiti wake juzi, Jumamosi usiku, mjini Pretoria, Afrika Kusini.
Naye
Raojelina anatarajiwa kumwelezea Rais Kikwete kuhusu hali ilivyo katika Madagascar
na hasa kuhusiana na jitihada za kuandaa Uchaguzi Mkuu nchini ambao umekuwa unakumbwa
na changamoto kadhaa.