2013-07-23 08:06:14

Papa afunika Brazil!


Baba Mtakatifu Francisko Jumatatu tarehe 22 Julai 2013 amewasili nchini Brazil na kupokelewa na viongozi wa Serikali, Kanisa na umati mkubwa wa watu waliokuwa wamejipanga kwenye barabara mbali mbali za mji wa Rio de Janeiro, kiasi kwamba, wakati mwingine msafara wa Baba Mtakatifu ulilazimika kusimama ili kusalimia wananchi waliokuwa na shauku na kumwona Baba Mtakatifu Francisko.

Baba Mtakatifu anamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kumwezesha kufanya hija ya kwanza ya kitume kama Khalifa wa Mtakatifu Petro nchini Brazil ambayo imekuwa na uhusiano wa pekee na viongozi wa Kanisa hasa kutokana na imani na urafiki wao na kwamba, yuko mbele yao akigonga mlango wa mioyo yao, akitaka afunguliwe ili aweze kuishi pamoja nao katika kipindi hiki cha juma zima, kama sehemu ya Maadhimisho ya Juma la Vijana Duniani.

Baba Mtakatifu katika hotuba yake anasema, hana fedha wala dhahabu, bali ndani mwake ana mbeba Yesu Kristo na yuko kati yao kwa jina lake, ili aweze kuwashirikisha mwali wa upendo wa kidugu unaowaka katika mioyo ya wengi na kwamba, anamtakia kila mmoja wao amani ya Kristo! Baba Mtakatifu anawashukuru viongozi wa Serikali na wadau mbali mbali waliowezesha hija yake ya kichungaji nchini Brazil.

Amewasalimu na kuwapongeza Makleri nchini Brazil kwa huduma makini wanayotoa kwa ajili ya Familia ya Mungu nchini humo. Anasema, uwepo wake miongoni mwao unalenga kuwaimarisha ndugu zake katika imani, matumaini na mapendo yanayobubujika kutoka kwa Kristo mwenyewe.

Baba Mtakatifu anasema hija yake ya kichungaji inapania kuadhimisha Siku ya Vijana Duniani, inayompania fursa ya pekee kukutana na kuzungumza na vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia, wanaovutwa na Kristo Mkombozi. Hawa ni vijana wanaotafuta hifadhi katika Moyo wake Mtakatifu pamoja na kusikiliza ule wito wake unaowachangamotisha kwa kusema "Basi enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi".

Vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanazungumza lugha mbali mbali na kutoka katika tamaduni tofauti, lakini kwa pamoja wanashikamanishwa na matumaini yao kwa Kristo anayeweza kuzima kiu ya ukweli na upendo licha ya tofauti zinazojitokeza kati yao.

Yesu anatoa nafasi ya kuweza kujenga na kudumisha urafiki na vijana hawa, ili hatimaye, waweze kuwa ni wadau wakuu wa uinjilishaji unaopania kujenga na kudumisha umoja na mshikamano kati ya watu. Vijana wako tayari kujitosa kimasomaso kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake kwani wanatambua kwamba, kamwe hataweza kuwaangusha!

Baba Mtakatifu Francisko anasema, anapozungumza na vijana anatambua kwamba, anazungumza pia na wazazi, jumuiya na makanisa yao mahalia. Vijana ni tumaini la Jamii kwa sasa na kesho iliyo bora zaidi, changamoto ya kuhakikisha kwamba, wanathaminiwa na kutunzwa vyema, kama ilivyo mboni ya jicho! Vijana ni kama dirisha linaloruhusu mambo ya ulimwengu ujao kuweza kupenya, hali inayoibua changamoto nyingi.

Vijana wanahitaji nafasi, hivyo ni jukumu la Jamii kutoa fursa hizi: kiroho na kimwili, ili waweze kujenga msingi wa maisha yao; wakiwa na usalama na uhakika wa maisha kwa njia ya elimu makini; kwa kuwarithisha tunu msingi za maisha ya kiroho na kiutu. Kwa hakika vijana wanapaswa kupewa maisha bora, kwa kuamsha karama na vipaji walivyonavyo ili kushiriki katika mchakato wa ujenzi wa hatima yao ya maisha, wakiwajibika pia kwa ajili ya mafao ya wengi.

Baba Mtakatifu anahitimisha hotuba yake kwa kuwataka wahusika mbali mbali kuwa karibu na vijana ili kujenga urafiki utakaosaidia kuanzisha majadiliano na vijana. Upendo wake unawakumbatia na kuwafunika wananchi wote wa Brazil katika tamaduni na utajiri walio nao. Anasema, atapata nafasi ya pekee kwa ajili ya kusali na kuwaombea kwa Bikira Maria wa Aparecida, akiwaombea ulinzi na tunza ya kimama kwa ajili ya nyumba na familia zao. Baba Mtakatifu anawashukuru wananchi wa Brazil kwa mapokezi makubwa waliyomkirimia!







All the contents on this site are copyrighted ©.