2013-07-23 09:38:12

Maadhimisho ya Mwaka wa Imani na changamoto zake nchini Tanzania


Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania katika mahojiano maalum na Radio Vatican anasema kwamba, Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, utekelezaji wake unafanyika katika ngazi ya Majimbo na hapo Novemba, Maaskofu wote watakusanyika Mji mkongwe wa Bagamoyo kwa muda wa siku tatu, ili kuadhimisha Mwaka wa Imani. RealAudioMP3
Bagamoyo ni mahali ambapo Imani ya Kanisa Katoliki nchini Tanzania ilipata chimbuko lake.
Hii itakuwa ni fursa kwa Familia ya Mungu nchini Tanzania kufanya tafakari ya kina kuhusu Kanuni ya Imani kwa kuyahusisha makundi mbali mbali ndani ya Kanisa kadiri ya mahitaji na usomaji wa alama za nyakati. Changamoto kubwa iliyoko mbele ya Familia ya Mungu nchini Tanzania, ni toba na wongofu wa ndani kwa kumpatia Mwenyezi Mungu kipaumbele cha kwanza, kwa njia ya ushuhuda na utakatifu wa maisha. Waamini wanaendelea kuchangamotishwa kujikita katika: Sala, Tafakari ya Neno la Mungu na Matendo ya huruma, kama njia ya kumsogelea Mwenyezi Mungu katika hija ya maisha yao!
Askofu Ngalalekumtwa anasema wakati huu wa Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani, ujumbe kwa vijana ni kutubu na kumwongokea Mungu, kwani ujana kwa sasa umekuwa nongwa! Wanapaswa kujichunga ili kamwe wasiharibu ujana wao kwa maisha yasiyo adili. Vijana wanaendelea kukabiliana na changamoto za maisha: kiuchumi, kiimani, kimaadili na kiutu. Wengi wao hawana fursa za ajira na matokeo yake ni kujihusisha na vitendo ambavyo ni kinyume cha sheria, utu na maadili mema. Vijana wanapaswa kulelewa kiroho, wajengewe ujasiriamali na wapewe nafasi ya kujifunza ufundi ili waweze kujiajiri wenyewe.
Tanzania baada ya kukaa kwa amani na utulivu kwa takribani miaka 50, kwa siku za hivi karibuni imejikuta ikikabiliana na changamoto za uvunjifu wa misingi ya haki na amani ambayo imesababishwa na lugha za uchochezi, madhulumu na mashambulizi ya kidini, kiasi kwamba kuna baadhi ya viongozi na waamini wamepoteza maisha yao.
Kuna haja ya kusimama kidete kulinda na kudumisha haki msingi za binadamu. Uchochezi unaofanywa na watu wa nje kwa malengo yao binafsi udhibitiwe na kamwe vijana wasikubali kutumiwa na watu wenye nia mbaya kutokana na umaskini wao ili kuvuruga misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano wa kitaifa kwa kupokea “vijisenti” ili wafanye vurugu.
Askofu Ngalalekumtwa anawataka watu hao wanaotumia vibaya utajiri na mali yao, kuwajengea uwezo vijana badala ya kusababisha maafa na uvunjifu wa misingi ya haki, amani na utulivu.








All the contents on this site are copyrighted ©.