2013-07-22 08:48:29

Wamissionari wanatumwa kwenda kujifunza mahangaiko ya watu!


Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu, C.PP.S., limehitimisha mkutano wake mkuu kwa kujiwekea malengo wanayopaswa kuyatekeleza katika kipindi cha miaka sita yaani: 2013 hadi mwaka 2019. Ndani ya viunga vya Radio Vatican, tunaye Padre Felix Mushobozi, Katibu mkuu aliyemaliza muda wake anayejuza zaidi yale yaliyojiri katika mkutano mkuu wa ishirini, uliokuwa unafanyika mjini Roma. RealAudioMP3
Jumuiya ya Wamisionari wa Damu Azizi ya Yesu ni Ushirika wa Mashahidi wa Kristu wenye kutoka katika tamaduni tofauti ulimwenguni; kwa lengo la kuhamasisha majiundo mapya katika Kanisa na kwenye mazingira tunamoishi.
Kutokana na mwongozo huu, wajumbe wa mkutano mkuu wa 20 waliokutana mjini Roma kuanzia tarehe 8 hadi 19 mwezi Julai, 2013 wamemchagua Padre William Nordenbrock kutoka Kanda ya Cincinnati (Marekani), kuwa mkuu mpya wa shirika, baada ya Pd. Francesco Bartoloni kumaliza muda wake wa uongozi.
Kabla ya uchaguzi, mkutano mkuu uliweka bayana Dira itakayoongoza shirika kwa kipindi cha miaka sita ijayo, yaani kuandia 2013 hadi 2019.
Umoja: tunasisitiza maisha ya pamoja ili kama Wamisionari tuweze kuishi vema karama za kiutu na kiroho tulizotunukiwa na Mwenyezi Mungu. Tunajitahidi kuishi karama za shirika kwa ajili ya uenjilishaji na utume ndani ya Kanisa na ulimwengu.
Utume na Uinjilishaji: Upendo wa Kristo unaojidhihirika katika fumbo la Msalaba kwa kumwaga damu yake Azizi, ndio unaotubidiisha katika uenjilishaji na utume wetu popote tunapotumwa.
Utume wa Neno la Mungu: Hii ndiyo karama kuu ya shirika letu zinamojikita karama nyingine zote. Kwa maana hii ni kwamba sisi Utambulisho wetu ni Umissionari tukiwa na maana sisi ni wahubiri wa Neno la Mungu – Kwa maneno na kwa ushuhuda wetu tukijaribu kusikiliza na kujibu Vilio mbalimbali vya Damu ya Kristo:
Katika Uenjilishaji tunajitambua kuwa tumeitwa kupeleka Upatanisho ambao Kristo alikuja kuuleta mahali popote ambapo kuna mipasuko ya kila aina: kiroho, kimwili, kimaadili, kijamii, kisiasa, kiuchumi, katika mazingira na viumbe ambavyo Mwenyezi Mungu ametukabidhi vitumike kadiri ya mpango wake.
Upatanisho: Lengo letu ni kuhakikisha kuwa katika ulimwengu na kanisa Upendo na huruma ya Mungu vinawaletea watu Uponyaji na ukombozi. Magonjwa ya kila aina yaweze kupata tiba toka kwa Damu ya Yesu; Watu wa kila jamaa, lugha, kabila na taifa wanakombolewa kutoka utumwa wa shetani na ubabe wa kila aina.
Tunatumwa hasa kwenda hadi pembezoni mwa Jamii na Kanisa: Katika maana aliyoeleza Baba Mt. Francisko toka alipoanza utume wake kama Askofu wa Roma na Khalifa wa Mtakatifu Petro. Baba Mtakatifu alituhimiza kutoka katika sakristia zetu na kwenda huko ambako watu wenye vilio mbalimbali waliko.
Kwenda mpaka pembezoni mwa mwa jamii. Alihimiza kuwa na mtazamo wa kanisa kwa ajili ya maskini na walalahoi. Huu ndio wito na utume wa Wamisionari wa Damu Azizi ya Yesu.
Katika mkutano wetu tumeona kuwa kazi ya Umisionari itakuwa na ufanisi kama tutaifanya kwa ushirikiano wa karibu na walei – watu wa kawaida wanaomwamini Kristo na kushiriki utume wake kama Wabatizwa. Wao wako kwenye nafasi nzuri ya kuelewa uchungu wa maisha ya kawaida kuliko sisi makleri ambao mara nyingi tunahubiri toka juu ya mimbari bila kushuka chini na kuhisi matatizo ya watu wa kawaida.
Tunahimizwa basi kwenda kushiriki mahangaiko ya watu pale wanakoishi. Tunaitikia mwaliko wa Baba Mtakatifu Francisko aliposema mchungaji hana budi kwenda kushiriki harufu ya kondoo wa Bwana.








All the contents on this site are copyrighted ©.