2013-07-22 10:02:17

Vijana wanahamasishwa kujenga utamaduni wa amani


Umoja wa Mataifa kwa kushirikiana na Jopo la waandaaji wa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013, wanaendesha majadiliano ya kina miongoni mwa vijana kuhusu dhamana na wajibu wao katika medani ya uongozi katika mchakato wa maendeleo endelevu na amani.

Tarehe 23 Julai 2013, kunafanyika tamasha linaloongozwa na kauli mbiu “Vijana na Utamaduni wa Amani”. Katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa katika tamasha hili anawakilishwa na Bwana Ahmad Alhendawi. Katika majadiliano haya, kila Bara litakuwa na mwakilishi mmoja mmoja.

Juma la vijana kama alivyosema Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Sala ya Malaika wa Bwana, Jumapili tarehe 21 Julai 2013 kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican ni fursa makini ya kuwasikiliza na kuzungumza na vijana kutoka pande mbali mbali za dunia sanjari na kujifunza matarajio yao kwa sas ana kesho iliyobora zaidi.

Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani ni jukwaa linalotumiwa na Mama Kanisa kutoa fursa kwa vijana wanaotaka kukutana na Mwenyezi Mungu katika hija ya maisha yao ya kiroho. Ni vijana wanaopenda kukutana na walimwengu, lakini pia ni nafasi ya kuangalia undani wa maisha yao, tayari kujiwekea mikakati na malengo kwa ajili ya siku za usoni.

Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani tangu yaliyopoasisiwa na Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili miaka 28 iliyopita, yamekuwa ni chemchemi ya miito mitakatifu. Changamoto kubwa iliyoko mbele ya Jumuiya ya Kimataifa ni kuhakikisha kwamba, inawajibika kujenga, kuimarisha na kuboresha dunia ili iweze kuwa ni mahali pazuri zaidi pa kuishi.








All the contents on this site are copyrighted ©.