2013-07-22 09:54:58

Jibidisheni kuutafuta Mlango wa Imani


Mheshimiwa Padre Raymond Saba, katibu mkuu mpya wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, wakati wa hija ya maisha ya kiroho mjini Roma, Lourdes na Nchi Takatifu amesema, Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, kiwe ni kipindi cha kugundua upya, uzuri na nguvu ya imani. RealAudioMP3

Ni muda muafaka wa kujifunza kwa makini ili kuifahamu vyema imani kwa Kristo aliyezaliwa, akateswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Hili ndilo wazo msingi linalopaswa kuyaongoza Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, uliotangazwa na kuzinduliwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, sanjari na Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican na Miaka 20 tangu Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili alipochapisha kwa mara ya kwanza Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki.

Padre Raymond Saba anawaalika waamini kwa mara nyingine tena kumwomba Kristo aweze kuwaongezea imani na kwamba, hii inapaswa kuwa ni sala ya kila siku ya mwamini. Waamini wakikosa kumlilia Kristo ili awaongezee paji la imani, watajikuta kwamba, wanakuwa ni Wakristo wa majina, Wakristo ambao wanaridhika kuhudhuria Ibada ya Misa Takatifu kila Jumapili, lakini wanashindwa kumwilisha imani yao kwa Kristo na Kanisa lake katika matendo na uhalisia wa maisha ya kila siku!








All the contents on this site are copyrighted ©.