2013-07-19 09:35:03

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 16 ya Kipindi cha Mwaka C wa Kanisa


Mpendwa mwana wa Mungu, karibuni katika tafakari Neno la Mungu, masomo ya Dominika ya 16 ya mwaka C. Mama Kanisa leo ataka tutambue kipi kilicho cha msingi katika maisha maisha yetu kwa ujumla na hasa maisha ya ufuasi wa Bwana. Mwinjili Luka anaweka mbele yetu tukio la Bwana aliyetembelea kijiji cha Martha na Mariamu. RealAudioMP3

Jambo linatuongoza kutafakari Injili, ni zile hekaheka za kila Martha na Mariamu kila mmoja wao akijaribu kumkarimu Bwana anayeenda kuwatembelea. Katika heka heka zao kutajitokeza tofauti na hivi kila mmoja atahangaika kadiri ya vionjo au tunaweza kusema kipaji chake. Hapa ndipo kutakuwa chanzo cha fundisho atakalolitoa Bwana hapo baadaye.

Mpendwa msikilizaji, dada hawa wawili wamepata malezi katika familia moja lakini kila mmoja atajitokeza tofauti na mwingine haya ndiyo maajabu ya uumbaji. Ndiyo kusema katika tofauti zao tunapata kuonja uasilia wa mtu mmojammoja katika kuitikia wito wa Mungu hata kama mtu yuko katika jumuiya. Utofauti wao wawakilisha utajiri wa mwanadamu.

Mpendwa mwana wa Mungu, tunamwona Martha ambaye kwa tabia yake anaonesha umuhimu wa kutenda kimasomaso, yaani maisha ya kuhudumia wengine, wakati Mariamu anatangaza upande mwingine yaani maisha ya sala na tafakari ya ndani. Mariamu anatufundisha kusikiliza na hivi kwa njia hiyo anataka kuonesha upeo mwingine wa maisha ya mwanadamu yaani mawasiliano na Mungu. Kwa kuwatazama hawa ndugu tayari tunazo namna mbili katika maisha yetu kadiri ya Injili yaani KUTENDA na KUTAFAKARI. Namna hizi mbili zaweza kujenga swali: Je namna moja ni ya maana kuliko nyingine? Kwa hakika fundisho la Bwana latuambia kuwa mifumo hii miwili haipingani bali yakamilishana katika kufikia ukamilifu wa maisha yetu.

Mpendwa msikilizaji, bado twajiuliza mifumo hii yategemezana kwa namna gani? Hebu tuone, katika hali ya kawaida bila Martha Bwana asingetamani kwenda kuwatembelea hawa ndugu, maana kuwatembelea watu maana yake kuchota furaha na kupeleka furaha. Kwa nini mtu aende ambapo anajua hakuna huduma ya chakula, maongezi nk.

Kumbe basi, ukarimu ni muhimu sana. Jambo jingine linalotokana na huduma ya Martha ni kwamba Mariamu asingepata nafasi ya kumsikiliza Bwana kama Martha asingejitoa katika kuandaa meza. Kama angekuwa peke yake angewajibika kupika na kuandaa kwa ajili ya Bwana. Ndiyo kusema, huduma ya Martha inapata kusimikwa katika maneno ya Bwana akisema: Kama mimi niliye Bwana nimewaosha miguu basi nanyi mkanawishane ninyi kwa ninyi, na yule mkubwa kati yenu awe kama mdogo na anayetawala awe kama yule anayetumikia.

Mariamu anayesikiliza Neno la Mungu anasadikika kuchagua lililo bora zaidi ni kweli lakini kama tulivyoona linasimikwa katika msingi wa huduma ya Martha. Basi Bwana anataka kutufundisha kuwa na uwezo wa kuona kipi ni cha msingi na kwa namna gani kukifanyia kazi na zaidi sana wapi kinalenga katika safari nzima ya wokovu wa mwanadamu.

Kumbe, thamani ya huduma inasimika maisha yetu lakini pia huduma bila tafakari, shughuli zetu zote zitakuwa zimejaa utupu ambao si rahisi kuuziba na tokeo la utupu ni anguko la imani na jumuiya ya watu kwa ujumla. Mpendwa msikilizaji, katika maisha yetu lazima tutenge muda wa kuongea na Mungu tukiwa peke yetu au katika familia, ni lazima kuwa Mariamu mwingine!. Hii ndiyo maana ya Jumapili, ndiyo maana ya kupokea sakramenti, ndiyo maana ya sala za kila siku, ndiyo maana ya hija na yote yaambatanayo na maisha ya missioni. Tumsifu Yesu Kristo.

Tafakari hii imeletwa kwako na Pd Richard Tiganya Cpps







All the contents on this site are copyrighted ©.