Ajali mbaya ya bus yatokea kwa vijana Mahujaji wa WYD 2013- tokea French Guiyana
Jumatano, huko French Guiyana, ilitokea ajali mbaya ya bus lililokuwa likisafirisha
vijana Wafaransa , katika kuianza hija ya kuelekea Rio de Janeiro, kwa lengo la
kushiriki katika adhimisho la 28 la Siku ya Vijana ya Dunia WYD. Bus hilo liligongana
uso kwa uso na lori na kusababisha binti mmoja kufariki papo hapo na wengine watatu
hali zao zinatajwa kuwa mbaya. Alhamis, Baba Mtakatifu Francisko, mara baada
ya kupata habari hii ya kusikitisha, kiroho aliunganika katika mateso na majonzi ya
vijana hao na familia zao. Papa kupitia Katibu wa Vatican Kardinali Tarcisio Bertone,
alituma telegram ya rambirambi kwa Askofu wa Cayenne, kwa niaba ya Maaskofu wote
wa French Guiyana , ambamo ameonyesha masikitiko yake kwa ajali hiyo. Na ametoa
baraka zake za kipapa kwa kafara wote wa ajali, na pia kwa wale waliowasaidia vijana
baada ya ajali kutokea, na wote wale walioguswa na msiba huu. Ajali hiyo ilitokea
katika barabara kuu inayounganisha mji wa Saint Laurent du Maroni na mji wa Cayenne,
baada ya bus kusafiri umbali wa kilomita 12. Katika bus hilo kulikuwa na wasafiri
23. Taarifa zinasema, mjini Paris Ufaransa, Alhamis jioni, Kardinali Andre Vingt
Trois, wa Jimbo Kuu la Paris, aliongoza Ibada ya Misa katika Parokia ya Mtakatifu
Leonè ambako kafara wa ajali wanatokea kwa nia ya kumwombea Marehemu na wote waliodhurika
katika ajali hii na familia zao. Vivyo hivyo Askofu wa Cayenne, aliongoza Ibada ya
Misa katika Kanisa kuu la Cayenne kwa nia hiyo ya kuwaombea kafara.