Jumuiya ya Kimataifa imeadhimisha Siku ya Nelson Mandela Kimataifa kwa sala na shughuli
mbali mbali kwa muda wa dakika 67, muda ambao Mzee Madiba aliutumia kwa ajili ya huduma
kwa wananchi wa Afrika ya Kusini. Ni kielelezo makini cha kiongozi ambaye amejipambanua
kwa kupinga ubaguzi wa rangi, nyanyaso na dhuluma, kiasi cha kusimama kidete kuanzisha
mchakato wa upatanisho, haki na amani.
Rais Jacob Zuma wa Afrika ya Kusini
anasema kwamba, hali ya Mzee Madiba bado si shwari sana. Amewashukuru wananchi wa
Afrika ya Kusini na Jumuiya ya Kimataifa katika ujumla wake kwa kumsindikiza Mzee
Madiba kwa sala, tangu alipolazwa Hospitalini hapo tarehe 8 Juni 2013.
Rais
Barack Obama wa Marekani ni kati ya viongozi wa Jumuiya ya Kimataifa waliotuma salam
na matashi mema kwa Mzee Madiba anapoadhimisha Miaka 95 tangu alipozaliwa. Anasema,
anaikumbuka ziara yake aliyoifanya hivi karibuni Nchini Afrika ya Kusini na kwamba,
aliguswa zaidi alipotembelea Kisiwa cha Robben, mahali ambako Mzee Nelson Mandela
alifungwa kizuizini kwa miaka 27.