Padre William Nordenbrock, C.PP.S. achaguliwa kuwa Mkuu wa Shirika la Wamissionari
wa Damu Azizi ya Yesu duniani: 2013 - 2019
Wajumbe wa mkutano mkuu wa 20 wa Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi ya Yesu wamemchagua
Mheshimiwa Padre William Nordenbrock kutoka Kanda ya Cincinnati, Marekani, kuwa Mkuu
mpya wa Shirika. Padre Nordenbrock anachukua nafasi ya Mheshimiwa Padre Francis Bartoloni,
aliyemaliza muda wake.
Takwimu za Shirika la Wamissionari wa Damu Azizi zinaonesha
kwamba, hadi kufikia Mwezi Mei 2013, kulikuwa na jumla ya Wanashirika 562, wanaoishi
na kutekeleza utume wao katika nchi 22. Barani Afrika Wamissionari wa Damu Azizi ya
Yesu wanafanya kazi nchini Tanzania na Guinea Bissau. Mkutano mkuu wa 20 umefafanua
dira itakayoongoza Shirika kuanzia mwaka 2013 hadi mwaka 2019.
Katika Ibada
ya Misa Takatifu iliyofanyika kwenye Kikanisa cha Makao Makuu ya Kanda ya Italia,
mjini Roma na kuongozwa na Mheshimiwa Padre William Nordenbrock, aliwaalika kwa namna
ya pekee Wamissionari wa damu Azizi ya Yesu, kujichotea huruma kutoka kwa Mwenyezi
Mungu kwani hiki ni kiini cha upendo unaojenga na kudumisha mshikamano wa dhati kati
yao na Mwenyezi Mungu.
Amemshukuru Padre Francis Bartoloni aliyempatia fursa
ya kujifunza mengi kutoka kwake kama Mkuu wa Shirika Msaidizi. Ni matumaini yake kwamba,
hazina na utajiri aliojichotea utamsaidia kutekeleza dira na mwelekeo wa Shirika katika
kipindi cha miaka sita ijayo.
Katika mahubiri yake Mheshimiwa Padre Francis
Bartoloni amewashukuru wajumbe wa mkutano mkuu wa Shirika kwa kazi nzuri walioifanya,
huku wakionesha moyo wa upendo na mshikamano wa dhati. Katika kipindi chote cha uongozi
wa ngazi ya juu Shirikani, amejifunza kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Mungu,
Kanisa na Shirika katika ujumla wake; ameonja upendo na uvumilivu kutoka kwa Wanashirika
wenzake, lakini bado kuna changamoto kubwa ya kuendelea kujifunza mahangaiko ya watu,
ili kujibu kilio cha damu kwa watu wa nyakati hizi.
Anawataka Wamissionari
kumwilisha changamoto inayoendelea kutolewa na Baba Mtakatifu Francisko ya kutoka
waliko, ili kuwaendelea wale ambao wamesukumizwa pembezoni mwa Jamii kutokana na uwepo
wa dhambi, athari za utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia.
Ni
mwaliko wa kuwa kweli ni vyombo vya upatanisho unaolenga kuleta mageuzi ulimwenguni
na katika Kanisa. Tasaufi ya Damu Azizi ya Yesu, iwe ni dira itakayowawezesha kutekeleza
dhamana hii kwanza kabisa kwa kujikita katika maisha ya Sala, Tafakari ya Neno la
Mungu pamoja na kusikilizana.
Padre Francis Bartoloni ambaye kabla ya kuchaguliwa
kwake kuwa Makamu mkuu wa Shirika na baadaye kuwa mkuu wa Shirika, aliishi na kufanya
utume wake nchini Tanzania katika Majimbo ya Singida, Dodoma, Morogoro na hatimaye
Jimbo kuu la Dar es Salaam amsema, kwa sasa yuko tayari kupokea utume mwingine kadiri
ya mapenzi ya wakuu wake wa Shirika.
Mara baada ya mahubiri, Padre Francis
alimkabidhi Padre William Nordenbrock mshumaa wa Shirika, tayari kuwaingiza Wanashirika
katika awamu nyingine ya uongozi huku wakitembea katika Mwanga wa Kristo Mfufuka.
Padre Bill kama anavyoitwa na wengi, alikiri Kanuni ya Imani na baadaye Ibada ya Misa
Takatifu ikaendelea kama kawaida.