2013-07-15 07:59:10

Hata wavuvi wanasubiri kusikia Habari Njema ya Wokovu!


Chukua nyavu zako tweka hadi kilindini, ndiyo kauli mbiu inayoongoza Maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria wa Mlima Karmeli, Msimamizi wa Mabaharia inayoadhimishwa na Mama Kanisa kila mwaka ifikapo tarehe 16 Julai. RealAudioMP3

Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania katika Maadhimishi haya sanjari na Mwaka wa Imani, wanawaalika waamini kwa namna ya pekee, kuhakikisha kwamba, Yesu kristo anakuwa ni kiini cha maisha na shughuli zao za kila siku na kwa njia hii, wanaweza kupokea changamoto kutoka kwa Kristo anayewataka kutweka hadi kilindini licha ya kazi kubwa waliyoifanya usiku kucha lakini wakaambulia patupu!

Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania, linapenda kuwashirikisha Mabaharia ile furaha ya imani kwa Kristo na Kanisa lake, kama sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji Mpya, dhamana ambayo inavaliwa njuga na Mama Kanisa katika Mapambazuko ya Millenia ya Tatu ya Ukristo. Waamini na watu wote wenye mapenzi mema wanaalikwa kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Inasikitisha kuona kwamba, Mabaharia wengi wananyanyaswa na kudhulumiwa na kwamba, utu na heshima yao wakati mwingine havipewi kipaumbele cha kwanza, bali watu wanaangalia zaidi faida inayozalishwa na Mabaharia hawa, hata kama inawagharimu maisha na utu wao! Hapa Waswahili wangeweza kusema, “Punda afe lakini mzigo ufike”.

Maaskofu wanabainisha kwamba, utume wa Bahari unaotekelezwa na Mama Kanisa kwa miaka mingi sasa unapania kwa namna ya pekee kabisa kuwasaidia waamini katika hija ya maisha yao ya Imani kwa Kristo na Kanisa lake. Ni utume unaolenga kuwasaidia Mabaharia kukabiliana na fursa, changamoto na matatizo wanayokumbana nayo kila siku wanapotekeleza wajibu wao.

Kwa njia ya ushuhuda wa upendo na mshikamano, Kanisa pia linapenda kuwahimiza waamini kuzisaidia familia za Mabaharia ambazo mara nyingi zinakabiliwa na hali ngumu ya maisha. Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania linakumbuka changamoto zilizotolewa na Washiriki wa Kongamano la ya 23 la Utume wa Bahari lililofanyika mjini Roma, Mwezi Novemba, 2012, kwa kukazia utume wa Kanisa katika kuwahudumia Mabaharia na mwaliko kwa Jumuiya ya Kimataifa kuhakikisha kwamba, wahusika wanaendelea kuboresha hali ya maisha ya Mabaharia pamoja na vitendea kazi vyao.

Mwishoni, Maaskofu wa Hispania wanasema, wanapenda kumwilisha katika vipaumbele vyao vya shughuli za kichungaji, changamoto inayotolewa na Baba Mtakatifu Francisko ya kutoka katika ubinafsi wao na kuanza kujimwaga pembezoni mwa Jamii kwa ajili ya kuwainjilisha wale wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii ili nao pia waweze kuonja ile furaha ya kuwa ni wafuasi wa Yesu.

Kwa tukio hili, waamini wanachangamotishwa kwenda kwenye fukwe za bahari ili kuwainjilisha hata Mabaharia kwa njia ya ushuhuda wa maisha amini na matakatifu. Mabaharia wanaonesha moyo wa matumaini ya kutaka kukutana na Yesu Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu; Kristo anayetangazwa na kushuhudiwa na Mama Kanisa katika maisha na utume wake, hasa miongoni mwa wale wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.








All the contents on this site are copyrighted ©.