2013-07-11 08:09:06

Mkakati wa maboresho ya elimu nchini Hispania


Baraza la Maaskofu katoliki Hispania hivi karibuni limehitimisha mkutano wake wa mia mbili na ishirini na nane, uliojadili pamoja na mambo mengine, taarifa ya Tume ya Elimu na Katekesi ya Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania katika mkakati wa maboresho ya elimu. RealAudioMP3

Maaskofu wamepembua pia taarifa ya Jumuiya ya Kimataifa kuhusu afya n avigezo vya elimu ya uzazi salama. Huu ni mwongozo uliotolewa kwa ajili ya wadau wanaojihusisha na uundaji wa sera za elimu na masuala ya afya.

Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania limeonesha wasi wasi wake kutokana na mapungufu makubwa yaliyojitokeza kwenye mwongozo huu, unaopaswa kutumiwa na nchi za Ulaya. Vigezo vilivyotolewa, havigusii hata kidogo kanuni maadili na utu wema, mambo msingi yanayopaswa kuzingatiwa na wadau wa elimu na afya, katika mchakato wa kumhudumia mtu mzima.

Baraza la Maaskofu kwa kuguswa na changamoto hizi, limeamua kuanza kuandaa hati ambayo itaihusisha Jumuiya ya Kikristo mintarafu kweli za kweli za Kiinjili, tunu msingi za maisha na wito wa ndoa na familia, kama sehemu ya majiundo ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Baraza la Maaskofu limepitia pia kanuni msingi zinazopaswa kutekelezwa na taasisi za Kanisa katika huduma ya elimu na afya. Kanuni hizi zitafanyiwa kazi katika mkutano wa Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania, kwenye mkutano wao ujao. Wanaangalia pia jinsi ya kukabiliana na changamoto za kimaadili na utu wema katika masuala ya elimu na afya kwa kuunda Tume moja ya Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania itakayokuwa na wajibu wa kutoa ushauri katika masuala nyeti ya elimu, afya na jamii. Wanaangalia pia uwezekano wa kuunda Tume ya Uinjilishaji Mpya na Katekesi.









All the contents on this site are copyrighted ©.