2013-07-11 08:29:39

Askofu mkuu Lebulu: haki, amani na upatanisho ni chanda na pete!


Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa Kumi na sita, katika Waraka wake Dhamana ya Afrika anabainisha kwamba, Kristo katika moyo wa maisha ya Kiafrika anapaswa kuwa ni chemchemi ya upatanisho, haki na amani na kwamba, Kanisa lina mchango wa pekee kabisa Barani Afrika katika kuhamasisha na kumwilisha tunu hizi msingi katika maendeleo na ustawi wa Bara la Afrika. RealAudioMP3

Upatanisho na haki ni mhimili mkuu wa amani ambayo kimsingi ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Hii ni amani inayobubujika katika haki, ukweli na upendo unaojenga na kuimarisha kifungu cha upendo na udugu katika Familia ya Mungu inayowajibika. Haki inafumbatwa katika fadhila ya ukweli.

Ni changamoto inayotolewa na Askofu Mkuu Josephat Lebulu wa Jimbo kuu la Arusha, Tanzania. Anasema, amani inagusa undani na moyo wa mtu. Ni fadhila inayogusa mahusiano, upendo, ukweli na unyofu wa moyo. Amani inajikita katika kulinda na kutunza mazingira, ambayo ni sehemu ya kazi ya uumbaji ambayo Mwenyezi Mungu amemkabidhi mwanadamu kuyatunza na kuyaendeleza kwa ajili ya mafao ya sasa na kwa ajili ya kizazi kijacho.

Askofu mkuu Lebulu anasema kwamba, amani ni fadhila inayodai uwajibikaji wa kiuchumi, kijamii na kisiasa. Kukosa na kukoseana ni sehemu ya ubinadamu, kupatana na kusahau ni mwanzo wa hija ya maisha ya utakatifu na maendeleo endelevu, changamoto kwa watu kujenga ndani mwao utamaduni wa msamaha na upatanisho, kama kielelezo cha amani ya kweli!







All the contents on this site are copyrighted ©.