2013-07-10 11:42:03

Ukarimu ni sehemu ya tunu msingi za maisha ya kiroho!


Hija ya Kichungaji iliyofanywa na Baba Mtakatifu Francisko, Kisiwani Lampedusa, Kusini mwa Italia, Jumatatu, tarehe 8 Julai 2013 ni changamoto kwa viongozi wa kidini kutambua adha na mahangaiko ya mamillioni ya wakimbizi kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanaotafuta usalama wa maisha.

Ni watu wanaopaswa kuonjeshwa upendo na ukarimu; kwa kuheshimu na kuthamini utu wao kama binadamu walioumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Watu wajenge utamaduni wa ukarimu kwa kuwapokea wakimbizi na wahamiaji kama ndugu zao! Lakini kwa bahati mbaya, licha ya mateso na mahangaiko ya wakimbizi na wahamiaji hawa kutoka sehemu mbali mbali za dunia, wanapofika Barani Ulaya, wanabaguliwa na kunyanyaswa, hali ambayo inaongeza machungu katika maisha ya wakimbizi hawa.

Taarifa zinaonesha kwamba, kuna zaidi ya wakimbizi, wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum wapatao millioni arobaini, waliotawanyika sehemu mbali mbali za dunia.

Ni maneno ya Kardinali Rodrigues Maradiaga, Rais wa Shirikisho la Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki Kimataifa, Caritas Internationalis, wakati huu Jumuiya ya Kimataifa inapoendelea kufanya tafakari ya kina kama sehemu ya kuamsha dhamiri, ili hatimaye, kutambua na kuchukua hatua madhubuti ili kushughulikia tatizo la wakimbizi na wahamiaji wanaokufa maji wakati wakiwa njiani kutafuta hifadhi ya maisha Barani Ulaya.

Kardinali Maradiaga anasema, Mwezi Novemba mwaka huu, kutafanyika mkutano mkuu wa viongozi wa kidini wapatao 400 ili kuzungumzia dhana ya ukarimu mintarafu dini mbali mbali duniani, kwani kama viongozi wa kidini wanalo jukumu la kuwalinda na kuwakirimia wakimbizi, wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum. Ukarimu ni sehemu ya mafundisho na tunu msingi za maisha ya kiroho.







All the contents on this site are copyrighted ©.