2013-07-10 09:51:17

Rehema kutolewa wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013


Katika Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013 yanayoongozwa na kauli mbiu "Basi enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa ni wanafunzi" kuanzia tarehe 22 hadi tarehe 29 Julai 2013, sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani uliotangazwa na kuzinduliwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, Papa Francisko anapenda kuwaalika vijana na waamini katika ujumla wao, kujipatia rehema kamili na rehema ya muda kwa kutimiza masharti yaliyowekwa na Mama Kanisa.

Rehema kamili inaweza kupatikana mara moja kwa siku, ikiwa kama mwamini atatimiza mashari kwa kuungama, kupokea Ekaristi Takatifu na kusali kwa ajili ya nia za Baba Mtakatifu Francisko pamoja na kuwakumbuka marehemu waamini waliolala kwenye usingizi wa amani, wakiwa na tumaini la ufufuko wa wafu. Waamini wanaalikwa kufanya toba na wongofu wa ndani, ili kuweza kushiriki kikamilifu katika Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013.

Kwa waamini ambao hawaweza kuhudhuria katika Maadhimisho ya Vijana kihalali, wanaweza pia kupata rehema kamili, ikiwa kama watatimiza masharti yaliwekwa na Mama Kanisa, kwa kufuatilia matukio hayo kwa njia ya vyombo vya mawasiliano ya kijamii.

Kanisa linatoa pia rehema ya muda kwa waamini wote watakaotimiza masharti yaliyotajwa, kwa ajili ya kuombea mafanikio ya Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013, wakiwa na moyo wa toba na ibada; kwa kusali kwa Bikira Maria, Mama yetu wa Brazil pamoja na Watakatifu na wenyeheri wasimamizi wa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani.

Lengo ni kuombea uthabiti wa imani miongoni mwa vijana ili hatimaye, waweze kutembelea katika utakatifu wa maisha. Mapadre waliotubu na wenye moyo wa ibada wanaweza kutekeleza dhamana hii kwa ajili ya waamini wanaotaka kupata rehema kamili na rehema ya muda wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani.

Itakumbukwa kwamba, rehema ni ondoleo mbele ya Mungu adhabu za muda iliyostahiliwa kutokana na dhambi ambazo kosa lao lilikwishasamehewa. Kwa kutimiza masharti yaliyopangwa, mwamini anapata ondoleo hilo kwa ajili yake au ya marehemu kwa huduma ya Kanisa ambalo, kama msimamizi wa neema za ukombozi, anagawa hazina ya mastahili ya Kristo na ya Watakatifu.







All the contents on this site are copyrighted ©.