2013-07-10 08:53:19

Jamii za Kiafrika hazina budi kujipanga vyema ili kukabiliana na ongezeko la idadi ya wazee watakaohitaji huduma makini za Kijamii!


Baba Mtakatifu Francisko mara baada ya Sala ya Malaikawa Bwana, Jumapili iliyopita tarehe 7 Julai 2013, alitambua uwepo wa Wanajumuiya ya Mtakatifu Egidio, waliokuwa wanahudhuria mkutano wa waratibu wa Jumuiya za Mtakatifu Egidio kutoka Afrika na Amerika ya Kusini. RealAudioMP3

Mkutano huu umehudhuriwa na Queen Said, Mratibu wa Jumuiya ya Mtakatifu Egidio, Tanzania anayeelezea kwa kina na mapana yaliyojiri kwenye mkutano huo. Anasema, wamejadili mbinu mkakati wa kupambana na changamoto mbali mbali zinazoibuliwa katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia pamoja na kuangalia jinsi ya kupanua wigo wa utume wa Jumuiya ya Mtakatifu Egidio, ili iweze kuwafikia watu wengi zaidi.

Lengo la Jumuiya hii ni kutaka kuwa ni sauti ya wanyonge na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii; watu ambao utu na heshima yao inabezwa na kutwezwa. Maendeleo ya sayansi na tiba ya mwanadamu yamesaidia kuboresha hali ya maisha ya watu wengi duniani. Kwa sasa umri wa kuishi umeongezeka maradufu, ikilinganishwa na miaka kadhaa iliyopita. Hii ina maanisha kwamba, katika miaka michache ijayo, hata Bara la Afrika litakuwa na idadi kubwa ya wazee, watakaohitaji huduma mbali mbali za kijamii.

Queen Said anasema, umefika wakati kwa Jamii za Kiafrika kuanza kujipanga vyema, kwani kwa miaka mingi hili halikuwa ni tatizo kutokana na idadi ya wazee kuwa ni wachache kiasi kwamba, waliweza kuhudumiwa katika Familia na Koo zao. Mambo yana badilika kwa kasi, wazee wengi wanaanza kuachwa peke kutokana na sababu mbali mbali.

Kumbe, kuna haja ya kujipanga vyema, ili kuimarisha huduma kwa wazee kwa siku za usoni sanjari na kuimarisha tunu msingi za maisha ya kifamilia, ili wazee hawa waweze kufurahia uzee wao badala ya kutelekezwa kwenye nyumba za wazee au kuachwa wakitangaza tanga barabarani ili kujipatia riziki yao kana kwamba, hawakuwa na ndugu wala Jamaa!

Jumuiya ya Mtakatifu Egidio inaendelea kutoa huduma kwa wagonjwa wa Ukimwi kwa njia ya Mradi wake maarufu unaojulikana kama "The Dream" unaotoa dawa za kurefusha maisha kwa wagonjwa wa Ukimwi pamoja na kuhakikisha kwamba, wanapunguza maambukizi ya ugonjwa wa Ukimwi kutoka kwa Mama kwenda kwa Mtoto bila kusahau maboresho ya huduma ya lishe ili kujenga mwili uweze kupambana vyema na magonjwa nyemelezi.

Mradi wa "The Dream" Uko sehemu mbali mbali Barani Afrika na kwa namna ya pekee umeonesha mafanikio makubwa nchini Malawi. Nchini Tanzania, mradi huu unatekelezwa USA-Riva na Mkoani Iringa.







All the contents on this site are copyrighted ©.