2013-07-09 10:19:18

Wakimbizi na wahamiaji waguswa na uwepo na maneno ya Papa Francisko Kisiwani Lampedusa!


Hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu Francisko Kisiwani Lampedusa imelenga kuamsha tena dhamiri za watu ili waguswe na mateso pamoja na mahangaiko ya wakimbizi na wahamiaji wanaopoteza maisha yao baharini kwa kuwa na tumaini la maisha bora Barani Ulaya. Umefika wakati wa kuondokana na utandawazi usiojali na kukumbatia utandawazi unaojikita katika ukarimu na mshikamano wa upendo.

Baba Mtakatifu akiwa Kisiwani Lampedusa ametupa shada la maua baharini kwa ajili ya wale waliopoteza maisha yao wakiwa njiani kuja Barani Ulaya. Amepata fursa ya kuzungumza na wakimbizi pamoja na wahamiaji wengi wao wakiwa ni wale wanaotoka Barani Afrika. Baba Mtakatifu aliwashukuru wahamiaji waliompokea katika makazi yao na kuwahakikishia kwamba, lengo lake Kisiwani hapo lilikuwa ni kuwaombea na wao pia kumwombea yeye katika maisha na utume wake.

Baba Mtakatifu amesali hata kwa wale ambao kutokana na sababu mbali mbali hawakuweza kufika katika Ibada ya Misa Takatifu iliyohudhuriwa na umati mkubwa wa watu. Wakimbizi wamemwambia Baba Mtakatifu kwamba, wao wanatafuta hifadhi ya kisiasa kwani wamekimbia nchi zao kwa sababu za kisiasa na kiuchumi. Hadi kufika kwenye Kisiwa cha Lampedusa wamekumbana na vikwazo vingi; wamenyanyasika na kudhulumiwa njiani; wanaomba msaada kutoka katika nchi mbali mbali ili waweze kuanza tena safari ya maisha yao, wakiwa na matumaini mapya.

Wanatambua kwamba, Italia inabeba mzigo mkubwa wa wahamiaji kutoka sehemu mbali mbali za dunia, lakini ikisaidiwa na kuwezeshwa, maisha ya wahamiaji na wakimbizi yanaweza kuboreka zaidi, kuna haja ya kuwa na mshikamano!

Baba Mtakatifu kabla ya kuhitimisha Ibada ya Misa Takatifu amewashukuru kwa mara nyingine tena wananchi wa Kisiwa cha Lampedusa kwa mfano na ushuhuda wa upendo na ukarimu kwa wakimbizi na wahamiaji. Anawataka waendelee kuonesha moyo wa ukarimu kwa wale wanaotafuta kuboresha maisha yao, ili waweze kuonja ukarimu wao.







All the contents on this site are copyrighted ©.