Gesi asilia inalenga kupambana na baa la umaskini Tanzania, ni kwa ajili ya mafao
ya wote!
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete amesema kuwa jukumu
kubwa la gesi asilia nyingi iliyogunduliwa na inayoendelea kugunduliwa maeneo mbali
mbali nchini ni kuwatoa Watanzania katika umaskini. Aidha, Rais Kikwete amesema kuwa
ni lazima wananchi waweze kuona na kuthibitisha manufaa ya gesi hiyo kwa maendeleo
yao katika kipindi kifupi.
Pia Rais Kikwete amesema kuwa uchochezi wa baadhi
ya wanasiasa kuhusiana na gesi asilia iliyogunduliwa nchini ni changamoto ambayo,
hata hivyo, Serikali yake iko tayari kupambana nayo. Rais Kikwete alitoa msimamo huo
mwishoni mwa wiki iliyopita wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Mtendaji Mkuu
wa Kundi la Makampuni ya British Gas (BG) Bwana Chris Finlayson, moja ya makampuni
ambayo yamegundua gesi na yameanza kuwekeza katika uchimbaji wa raslimali hiyo muhimu.
Katika
mazungumzo hayo yaliyofanyika Ikulu, Dar Es Salaam, Rais Kikwete alimwambia Bwana
Finlayson na ujumbe wake kuwa gesi asilia hiyo inayoendelea kugunduliwa nchini ni
raslimali muhimu na lazima itumike katika “kuwatoa watu wetu katika umasikini na lazima
ibadilishe maisha yao.” Aliongeza Rais Kikwete: “Hivyo, maandalizi ya uchimbaji wake
yasichukue muda mrefu …..miaka 10 hivi….. huu ni muda mrefu sana kwa sababu wananchi
wetu wanahitaji kuona manufaa ya gesi asilia hiyo katika kipindi kifupi iwezekanavyo”.
Aliongeza
Rais Kikwete: “Ni dhahiri kuwa nyie wabia wetu mtanufaika na gesi asilia hiyo kutokana
na uwekezaji wenu lakini kimsingi tunataka gesi hii iwanufaishe watu wetu, iwatoe
katika umasikini. Kama gesi hiyo inaweza kutuingizia pato la dola za Marekani bilioni
moja kwa mwaka, ni dhahiri tunaweza kuibadilisha nchi hii ikawa mbingu.”
Kuhusu
wanasiasa wachochezi ambao wamekuwa wanawachochea wananchi wa Mtwara kudai kuwa gesi
isitoke katika Mkoa huo na kuwa itumike kwa manufaa yao pekee, Rais Kikwete alisema:“Uchochezi
wa wanasiasa ni changamoto. Hakuna shaka. Lakini hii ni changamoto ambayo Serikali
itapambana nayo na ina uwezo wa kutosha wa kumaliza changamoto hiyo.”
Naye
Bwana Finlayson alimweleza Rais maendeleo ya maandalizi ya uchimbaji wa gesi asilia
hiyo ikiwa ni pamoja na kutoa nafasi za masomo kwa vijana wa kitanzania kusomea utaalamu
mbali mbali wa gesi hiyo asilia.
JK: Tutafuta aibu ya kuagiza siagi na jibini
toka nje
Rais Jakaya Mrisho Kikwete amesema kuwa Serikali yake itaanza safari
ya kufuta aibu ya Tanzania kuendelea kuagiza siagi na jibini kutoka nje ya nchi wakati
kuna raslimali za kutosha kuzalisha bidhaa hizo hapa nchini. Hivyo, ameomba Uholanzi
kushirikiana na Serikali ya Tanzania na wadau wengine nchini kuleta mageuzi makubwa
katika sekta ya mifugo na sekta ndogo ya uzalishaji maziwa, kama hatua ya kwanza kuachana
na uagizaji wa bidhaa hizo ambazo zinaweza kuzalishwa nchini.
Rais Kikwete
amesema kuwa sambamba na mageuzi katika sekta ya mifugo, Serikali yake inataka kuongeza
kasi katika uwekezaji na uzalishaji wa maua na mazao mengine ya bustani hasa katika
maeneo yenye hali ya hewa ya kustawisha mazao hayo kama Nyanda za Juu Kusini.
Rais
Kikwete ameyasema hayo Jumatatu, Julai 8, 2013 Ikulu, Dar Es Salaam wakati alipokutana
na Balozi wa Uholanzi nchini, Mheshimiwa Dkt. Ad Koekkoek ambaye amemaliza muda wake
na alikuwa anamwaga Rais. Katika mazungumzo hayo, Rais Kikwete amemshukuru Balozi
Koekkoek kwa “kuufikisha uhusiano wetu kwenye ngazi za juu kabisa za mahusiano ya
kimataifa” na kumtaka aendelee kuunga mkono jitihada za maendeleo ya Tanzania popote
atakapokuwa baada ya kustaafu.
Rais amemwambia Balozi kuwa Tanzania inataka
kuendeleza sekta ya uzalishaji maziwa nchini na bidhaa zinazotokana na maziwa ikiwa
ni pamoja na siagi na jibini. “Kuagiza siagi na jibini kutoka nje ya nchi ni jambo
halina maelezo ya kutosha wala kuridhisha wakati tunazo raslimali zote za kutosha
kuzalisha bidhaa hizo hapa nchini.”
“Tunataka kuleta mageuzi makubwa katika
sekta hii na tunaomba Serikali ya Uholanzi kuwa mbia wetu mkubwa kwa sababu siyo tu
kwamba ina uzoefu wa miaka mingi na ujuzi mkubwa wa eneo hili, lakini pia ni soko
muhimu wa bidhaa za maziwa kama ilivyo soko la bidhaa za maua.”
Wakati huo
huo, Rais Kikwete amekutana na kufanya mazungumzo na Spika wa Bunge la Korea Kusini
Mhe. Hee Chang na ujumbe wake. Mazungumzo hayo yamefanyika Ikulu, Dar Es Salaam. Katika
mazungumzo hayo, Mheshimiwa Hee Chang amesifu mafanikio makubwa yaliyopatikana chini
ya uongozi wa Rais Kikwete akisisitiza kuwa Tanzania ina nafasi ya kuweza kupiga hatua
kubwa za maendeleo katika miaka ijayo kama itaendelea na kasi ya sasa ya maendeleo
na kukua kwa uchumi.
“Miaka 50 iliyopita, Korea Kusini ilikuwa nchi masikini
kabisa pato la wastani la kila Mkorea likiwa ni dola za Marekani 80 tu. Katika miaka
30 hadi 40, hata hivyo, tumefanikiwa kupiga hatua ya maendeleo na tuko tayari kutumia
uzoefu wetu wa kukabiliana na changamoto za maendeleo kusaidiana na Tanzania, nchi
ambayo ina kila dalili za kuleta mageuzi ya haraka katika kiwango chake cha maendeleo.”
Amesema Spika huyo na kuongeza: “Tanzania ni mbia wetu wa kiuchumi na tunataka kusema
kuwa kama mkikabiliwa na tatizo la kiuchumi ama la kimaendeleo ambalo tunaweza kulitatua
kwa uwezo wetu mdogo, tunawakaribisha sana. Tuko tayari kushirikiana na kufanya kazi
nanyi.”
Naye Rais Kikwete ameishukuru Korea Kusini kwa mchango wake katika
maendeleo ya Tanzania katika nyanja mbali mbali ukiwamo ujenzi wa Daraja la Malagarasi
(Daraja la Kikwete) ambao uko kwenye hatua za mwisho kukamilika. “Daraja lile ni ishara
kubwa ya urafiki kati ya Tanzania na Korea Kusini. Ni daraja ambalo limefungua mawasiliano
ndani ya nchi yetu na ni daraja ambalo limefungua mawasiliano kati ya Tanzania na
nchi za Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC). Tunawashukuru sana.”