2013-07-09 09:59:14

Asante Papa Francisko kwa kuwa ni chombo cha amani, njaa na kiu ya watu wanaoteseka na mawimbi mazito baharini!


Moyo wangu wamtukuza Bwana na roho yangu inamshangilia Mungu Mkombozi wangu, kwa kuwa amewatembelea watu wake. Ni wimbo wa sifa na shukrani uliotolewa na Askofu mkuu Francesco Montenegro, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Agrigento, Kusini mwa Italia, mara baada ya Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu iliyoongozwa na Baba Mtakatifu Francisko, kwenye Kisiwa cha Lampedusa alikokwenda kusali na kutoa heshima kwa wahamiaji na wakimbizi wanaopoteza maisha yao baharini wakiwa safarini kwenda Barani Ulaya.

Lampedusa kimekuwa ni Kisiwa cha Matumaini na Kifo, kwani hapa kuna wakimbizi na wahamiaji kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanatia nanga ya matumaini kwa leo na kesho iliyo bora zaidi. Ni mahali ambapo watu wanaonja adha ya utumwa, nyanyaso na madhulumu ya kila aina, lakini bado wanapiga moyo konde kutafuta uhuru na maendeleo ya kweli, lakini kwa bahati mbaya, wengi wao wanapoteza maisha wakiwa baharini hata kabla ya kufika Kisiwani hapo.

Askofu mkuu Francesco Montenegro anasema, Kisiwa cha Lampedusa ni mahali ambapo watu wanatafuta haki na utu wa mwanadamu unaopaswa kulindwa na kuheshimiwa. Kuna haja ya kujenga utamaduni wa ukarimu, upendo na mshikamano wa kweli kwa nchi hizi ambazo kwa miaka mingi zilitambulikana kuwa ni tajiri, lakini leo hii zinakumbana na umaskini wa hali na kipato!

Waamini wa Jimbo kuu la Agrigento wanamshukuru Baba Mtakatifu Francisko kwa kuendelea kuwa ni chombo cha amani na njaa pamoja na kiu ya haki kwa wote wanaoteseka sehemu mbali mbali za dunia; hawa ni watu wanaopaswa kuonjeshwa mawimbi ya upendo na ukarimu.







All the contents on this site are copyrighted ©.