Waseminari na Wanovisi wanapaswa kuwa ni wajumbe wa faraja, wanaobeba Msalaba wao
kwa imani na matumaini katika sala na utume!
Baba Mtakatifu Francisko katika mahubiri yake kwenye Ibada ya Misa Takatifu, Jumapili,
tarehe 7 Julai 2013, wakati wa kufunga Maadhimisho ya Siku ya Waseminari na Wanovisi,
kama sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, amewapongeza vijana hao katika hija
ya maisha inayowapatia fursa kugundua, kuhakiki na kuimarisha wito wao kwa njia ya
majiundo makini.
Vijana hawa wanapaswa kutambua kwamba, wanaitwa na Kristo
mwenyewe ili kushiriki utume wa kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia.
Liturujia ya Neno la Mungu, Jumapili ya kumi na nne ya kipindi cha Mwaka wa Kanisa
inakazia mambo makuu matatu: furaha katika faraja, Msalaba na umuhimu wa sala.
Baba
Mtakatifu amewaambia Waseminari na Wanovisi waliofurika kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu
Petro mjini Vatican kwamba, hata katika mahangaiko yao ya ndani, Mwenyezi Mungu anaweza
kuwakirimia faraja na kubembelezwa kama Mama mzazi afanyavyo kwa mtoto wake. Kila
mwamini anaalikwa kuwa mjumbe wa matumaini kwa wale waliokata tamaa.
Ili kufanikisha
utume huu, waamini wenyewe wanapaswa kuonja faraja na furaha inayobubujika kutoka
kwa Mwenyezi Mungu. Huu ndio utume ambao waamini wanapaswa kuutekeleza katika maisha
yao kwa njia ya ushuhuda wa maisha yanayoburudisha mioyo ya wale waliokata tamaa,
ili kuamsha tena matumaini mapya yanayopata chimbuko lake kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
Baba Mtakatifu amewaambia Waseminari na Wanovisi kuhusu umuhimu na ukuu wa
Fumbo la Msalaba, yaani mateso, kifo na ufufuko wa Kristo kutoka katika wafu, kielelezo
cha ushindi mkuu. Kama ilivyokuwa kwa Mitume wa Yesu, hata wao watakabiliana na Fumbo
la Msalaba katika maisha na utume wao, utakaowawezesha kuzaa matunda yanayokusudiwa
katika shughuli za kichungaji mintarafu mantiki ya Kristo mfufuka. Ni mwaliko wa kujitoa
katika ubinafsi, tayari kujitosa kimasomaso kutangaza upendo wa Kristo. Msalaba wa
Kristo ni kielelezo cha ushindi, huruma na upendo wa Mungu unaomwezesha mwamini kuwa
ni kiumbe kipya.
Baba Mtakatifu anawaalika Waamini kusali bila kuchoka kwa
ajili ya watenda kazi katika shamba la Bwana. Ni changamoto kwa watawa kujenga na
kudumisha utamaduni wa kupenda kusali daima, kama alivyokazia Baba Mtakatifu mstaafu
Benedikto wa kumi na sita wakati wa utume wake. Utume ni matokeo ya sala, mwanga na
nguvu ya kuweza kusonga mbele. Kanisa halitaweza kupata mafanikio makubwa ikiwa kama
halitaweza kujishikamanisha na Kristo kwa njia ya sala na tafakari ya kina, chemchemi
ya maisha na utume wa Kanisa.
Baba Mtakatifu anakumbusha kwamba, Uinjilishaji
unafanyika kwa njia ya kupiga magoti, mwaliko kwa Waseminari na Wanovisi kuwa kweli
ni watu wa sala, vingine utume wao utakuwa sawa na ajira zinazopatikana duniani. Yesu
alikuwa ni mtu wa sala, daima alijitenga na watu akapata muda wa kusali kabla ya kufanya
matukio makubwa katika maisha yake, changamoto endelevu kwa Mapadre na Watawa kujenga
utamaduni wa kufanya tafakari ya kina na kujiachilia mikononi mwa Mwenyezi Mungu ili
aweze kuwaongoza kwa mwanga wa Roho Mtakatifu. Msalaba uwe ni dira na mwongozo wa
maisha na utume wao!