2013-07-08 07:57:01

Papa Francisko ni mjumbe wa amani, matumaini na mshikamano wa mapendo!


Askofu mkuu Francesco Montenegro wa Jimbo kuu la Agrigento lililoko Kusini mwa Italia anasema, hija ya kichungaji ya Baba Mtakatifu Francisko ni tukio la furaha na neema kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Uamuzi wa Baba Mtakatifu kutembelea na kusali na wananchi wanaoishi katika Kisiwa cha Lampedusa ni ujumbe wenye nguvu na mwaliko wa kusoma alama za nyakati kwa jicho la Kimungu.

Kisiwa cha Lampedusa kwa miaka mingi kimekuwa ni alama ya matumaini kwa wahamiaji na wakimbizi kutoka Barani Afrika wanaotaka kusalimisha maisha yao. Baadhi yao wanatafuta jinsi ya kuboresha maisha yao wakiwa Italia na Ulaya katika ujumla wake.

Dhana ya uhamiaji inabeba ndani mwake anasema Askofu mkuu Montenegro mateso na mahangaiko ya ndani; hiki ni kilio cha watu wanaotafuta haki na amani. Kundi hili ni kubwa kiasi kwamba, watu hawawezi kukaa kimya kana kwamba, hakuna kinachotendeka kwa maelfu ya watu wanaoendelea kuteseka na kufa maji baharini.

Uwepo wa Baba Mtakatifu Francisko kisiwani hapa ni changamoto kwa wadau mbali mbali kujifunga kibwebwe kwa njia ya msingi wa Injili, ili: uhuru, haki na amani viendelee kutawala sehemu mbali mbali za dunia. Baba Mtakatifu anapenda kuwaimarisha waamini katika kutekeleza wajibu wao wa Kikristo kwa kuwaonjesha jirani zao upendo na ukarimu.

Askofu mkuu Francesco Montenegro wa Jimbo kuu la Agrigento anasema kwamba, waamini na watu wenye mapenzi mema Jimboni mwake, wamejiandaa kiroho na kimwili kwa ajili ya hija ya mshikamano inayofanywa na Baba Mtakatifu Francisko Jimboni humo.








All the contents on this site are copyrighted ©.