2013-07-06 09:02:41

Usalama barabarani! Unawajibishwa kiimani!


Ajali barabarani ni kati ya vyanzo vikuu vya vifo na ulemavu miongoni mwa vijana wengi Barani Ulaya. Ajali barabarani zinachangia kuharibika kwa haraka kwa vyombo vya usafiri na miundo mbinu inayogharimu kiasi kikubwa cha fedha za walipa kodi. RealAudioMP3

Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, linawaalika watumiaji wa vyombo vya usafiri kuhakikisha kwamba, wanakuwa makini katika matumizi ya barabara ili kulinda na kuokoa maisha, vyombo vya usafiri na miundo mbinu. Wanawauliza watumiaji wa vyombo vya usafiri na barabara, “Je, unapoendesha ni mwanga gani unaokuongoza? Imani inakuwajibisha katika kuendesha”.

Maaskofu Katoliki Hispania wanawakumbusha waamini na wananchi kwa ujumla kwamba, wanapaswa kuongozwa na imani katika matumizi bora ya vyombo vya usafiri, ili kuokoa, kulinda na kudumisha Injili ya Uhai; vyombo vya usafiri pamoja na miundo mbinu.

Sehemu hii ya Ujumbe wa Baraza la Maaskofu ni changamoto katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Mtakatifu Kristofa, inayoadhimishwa kila Mwaka ifikapo tarehe 7 Julai.

Watumiaji wa vyombo vya usafiri watambue kwamba, vyombo vyao ni madhabahu ndogo inayobebea Injili ya Uhai wa mwanadamu, kumbe, kwa jicho na fikara hizi za kiimani, wawe makini katika matumizi bora ya barabara. Uinjilishaji mpya unawachangamotisha waamini kuhakikisha kwamba, imani inakuwa ni dira na mwongozo katika hatua mbali mbali za maisha yao hapa duniani. Kila mtu anapaswa kuwajibika kuhusiana na maisha yake mwenyewe na yale ya jirani zake mbele ya Mwenyezi Mungu.

Watu wakumbuke kwamba, maisha ya mwanadamu ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu na kwamba, ni matakatifu yanapaswa kulindwa na kuendelezwa. Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania linaipongeza Serikali kwa kuchukua hatua za dharura ili kupunguza idadi ya ajali barabarani nchini humo na kwamba, kwa miaka ya hivi karibuni idadi ya ajali zimeendelea kupungua mwaka hadi mwaka.

Papa Paulo VI kunako mwaka 1978, akiwa nchini Hispania, aliwataka watumiaji wa barabara kuwa na busara sanjari na kuheshimu sheria za usalama barabarani; mambo msingi kwa watumiaji wa barabara.

Baraza la Maaskofu Katoliki Hispania linahitimisha ujumbe wake kwa Maadhimisho ya Kumbu kumbu ya Mtakatifu Kristofa msimamizi wa wasafiri hapo tarehe 7 Julai 2013 kwa kuwaweka wote chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria, nyota ya wasafiri.








All the contents on this site are copyrighted ©.