2013-07-06 10:28:34

Mmechaguliwa kwa jicho la Kristo, endeleeni kufundwa na Kristo pamoja na Kanisa lake!


Baba Mtakatifu Francisko katika Waraka wake wa kwanza wa kichungaji, Mwanga wa Imani anasema, Maadhimisho ya Siku za Vijana Duniani ni mahali ambapo vijana wanapata fursa ya kushuhudia imani kwa namna ya pekee kabisa na kwamba, hii ni changamoto kwao kuhakikisha kuwa wanajitahidi kuiishi imani hii kwa ukamilifu mkubwa. Ni mwaliko wa kutafuta utakatifu wa maisha! RealAudioMP3

Padre Beno Michael Kikudo wa Jimbo kuu la Dar Es Salaam katika mahojiano maalum na Radio Vatican, wakati huu Waseminari na Wanavisi wanapoadhimisha Siku yao kama sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani anapenda kuwaangalisha vijana hawa kwamba, kuna changamoto kubwa mbele yao, kwani mavuno ni mengi lakini watenda kazi katika shamba la Bwana ni wachache.

Hata katika uhaba wa miito mitakatifu ndani ya Kanisa, Waseminari na Wanovisi wanapaswa kuishi utakatifu wa maisha kwani huu ndiyo mwaliko wa kwanza kabisa. Vijana watambue wajibu na dhamana iliyoko mbele ya maisha yao, jambo linalowachangamotisha kuwa waaminifu, wakweli na wa wazi, mambo ambayo yanafumbatwa katika utakatifu wa maisha.

Wanapaswa kujiandaa vyema kwa kukazia vipaumbele vinavyotolewa na Mama Kanisa katika majiundo ya elimu dunia, maisha ya kiroho, kiutu na kichungaji. Watambue kwamba, majiundo ni mchakato endelevu, wao wanapaswa kujenga utamaduni wa kusikiliza kwa makini mintarafu mahitaji ya Kanisa, daima wakisoma alama za nyakati. Wazame na kuchagua fungu lililo bora, tayari kuwashirikisha wengine. Waseminari na Wanovisi watambue kwamba, wamechaguliwa kwa jicho la Kristo, waendelee kufundwa na Kristo mwenyewe!







All the contents on this site are copyrighted ©.