2013-07-05 09:08:42

Mavuno ni mengi, watenda kazi bado hawatoshi!


Jimbo kuu la Dar es Salaam linamwimbia Mwenyezi Mungu utenzi wa sifa na shukrani kwa ajili ya zawadi ya Mapadre wapya na wale wa Shirika la Wakarmeli na Wasalesiani wa Don Bosco waliopewa Daraja Takatifu la Upadre, Ijumaa tarehe 5 Julai 2013 na Askofu Msaidizi Titus Joseph Mdoe wa Jimbo kuu la Dar Es Salaam. Ibada hii imefanyika kwenye Parokia ya Mbezi Louis, Kanisa la Mtakatifu Peter Claver. RealAudioMP3

Padre Beno Michael Kikudo wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam ambaye kwa sasa yuko kwenye hija ya maisha ya kiroho Lourdes, Ufaransa kama sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, katika mahojiano na Radio Vatican, anapenda kuchukua nafasi hii kuwakaribisha Mapadre wapya kwa moyo na mikono miwili, kwani mavuno ni mengi lakini watenda kazi katika shamba la Bwana ni wachache.

Jimbo kuu la Dar es Salaam kwa sasa lina jumla ya Parokia 77 zinazohitaji kuhudumiwa kwa karibu zaidi. Mapadre wapya watasaidia mchakato wa kuhakikisha kwamba, Familia ya Mungu Jimbo kuu la Dar es Salaam inapata huduma makini kwa wakati muafaka, changamoto kwa Mapadre wapya ni kuanza maisha na utume wao kwa kujishikamanisha na Kristo, bila kupunguza kasi!

Padre Beno Kikudo kwa namna ya pekee kabisa anayaelekeza macho na matumaini yake kwa Mafrateri 10 walioingia katika nyumba ya malezi, Mtongani, Jimbo kuu la Dar es Salaam tayari kuanza majiundo ya maisha na utume wa Kipadre. Anawaalika vijana hawa wote "kugangamara" na kamwe wasirudi nyuma kwani Kanisa lina matumaini nao!







All the contents on this site are copyrighted ©.