2013-07-05 08:23:45

Charukeni katika uzalishaji wa zao la Pamba!


Waziri Mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda amecharuka na kuwakemea viongozi na watendaji wakuu kwenye sekta ya pamba ambao wanawawonya wakulima wadogo kwa kuwazuia kutumia kilimo cha mkataba kama njia ya uhakika ya kupata soko kwa zao hilo.

Ametoa kauli hiyo Alhamisi, Julai 4, 2013 wakati akifungua Kongamano na Mkutano wa Kumi wa Wadau wa Sekta Ndogo ya Pamba ulioanza leo kwenye Chuo cha Benki Kuu jijini Mwanza. Mkutano wa siku mbili utamalizika kesho.

Alisema Chama cha Wakulima Pamba (TACOGA) hakina budi kusimamia mapinduzi ya kilimo cha pamba nchini kama kweli kinataka kuwasadia wakulima wadogo watoke hapo walipo na waboreshe maisha yao. “TACOGA na TCA (Chama cha Wafanyabiashara ya Pamba) kaeni pamoja na mfanye tathmini ya uundwaji wa taasisi hizi. Ni lazima muwe tayari kutetea maslahi ya wakulima wa zao hili na si vinginevyo... kama hamuwezi kulifanya hili basi hamstahili kuwepo,” alisema huku akishangiliwa na washiriki wa mkutano huo.

Waziri Mku alisema wadau wengi aliokutana nao wamependekeza kilimo cha mkataba kiendelee baada ya mapungufu yaliyojitokeza kufanyiwa kazi ikiwemo kutoa elimu ya mkataba kwa wadau wote na kusajili vikundi vya wakulima ili vitambulike kisheria.

“Naamini kabisa kuwa utaratibu huu wa kilimo cha mkataba, ukisimamiwa vizuri, utaleta mafanikio katika kuongeza tija; kuboresha ubora na usafi wa pamba, na hivyo kuifanya pamba ya Tanzania kurudia sifa iliyokuwa nayo ya kulipwa bei ya upendeleo (premium price), kuboresha huduma za ugani na kuzuia wakulima wasiendelee kupunjwa kupitia mizani,” alisema.

Aliwataka viongozi na wadau wengine waache kutetea maslahi binafsi katika jambo hilo na badala yake wazifanyie kazi changamoto zilizojitokeza ili zirekebishwe. “Ninawasihi tutengeneze mazingira ambayo yanampatia mkulima fursa ya kufikia uzalishaji mkubwa wenye tija ambao pia unampa nafuu ya maisha. Naiagiza, Bodi ya Pamba isimamie sheria katika utekelezaji wa kilimo cha mkataba,” alisisitiza.

“Kuna baadhi ya watu wenye uwezo wa kifedha hawautaki utaratibu huu kwani wamezoea kuwakopesha wakulima kwa riba kubwa wakati wa dhiki na kuja kuwadai wakishauza mazao yao... utaratibu huu unawapunguzia wateja kwani wakulima sasa watakuwa na utaratibu mbadala wa kupata mikopo nafuu kupitia mfumo huu wa kilimo,” alisema.

Waziri Mkuu alisema utaratibu wa kilimo cha mkataba katika zao la pamba unatekelezwa kwa ridhaa ya wadau wenyewe wa pamba waliokaa katika Mkutano wa Saba uliofanyika Juni 11, 2011 baada ya miaka mitatu ya ufanisi wa majaribio katika Mkoa wa Mara, Wilaya ya Bariadi (Simiyu) na Wilaya ya Kibondo (Kigoma).

Alisema kilimo hicho kinachosimamiwa na Tanzania Gastby Trust kupitia Program ya Kuendeleza Kilimo cha Pamba na Viwanda vya Pamba (CTDP) hapa nchini kinaelezewa kudhoofishwa na uwepo wa viongozi wachache katika maeneo yanayolimwa pamba wanaopinga au kuwashawishi wakulima kuukataa mfumo huo kwa maslahi yao binafsi.

“Katika maeneo mengine utakuta wakala wananunua pamba kutoka kwa wakulima waliokopeshwa pembejeo na CTDP bila ya wao kuwasaidia wakulima kwa hali yeyote wakati wa kilimo hivyo kufanya mfumo wa kurejesha mikopo hiyo uvurugike, na wakulima washindhwe kurudisha mikopo yao,” aliongeza.

Alisema hali hiyo ilisababishwa kilimo cha mkataba kisimamishwe katika msimu wa kilimo wa 2012/2013 na kuchangia kushuka kwa uzalishaji wa zao hilo.

Alisema licha ya kuwa zao la pamba linalimwa katika mikoa takriban 15 hapa nchini, bado kilimo cha zao hilo kinakabiliwa na changamoto nyingi zikiwemo tija ndogo katika uzalishaji wa pamba ambapo sasa hivi wastani wa Taifa wa uzalishaji ni kilo 300 kwa ekari ikilinganishwa na lengo lililowekwa la kufikia uzalishaji wa kilo 1,500 kwa ekari ifikapo mwaka 2015.

“Hali hii inatokana na wakulima wengi kutozingatia kanuni bora za kilimo cha pamba, huduma duni za ugani na utafiti, ukosefu wa pembejeo, mitaji na soko la uhakika wa zao hili pamoja na zana duni za kilimo. Uhaba wa viwanda vya kutosha kuongezea pamba thamani ni jambo ambalo pia linasababisha tuuze pamba ghafi katika soko la dunia ambalo bei yake mara kwa mara haitabiriki,” aliongeza.

Alisema changamoto nyingine ni bei ndogo ya pamba wanayopata wakulima kutokana na kuyumba kwa bei ya zao hilo katika soko la dunia. Ili kuondokana na tatizo hili, alisema wadau wamependekeza kuanzishwa kwa mfuko maalumu wa kufidia bei ya zao la pamba kwa wakulima pale bei zinaposhuka katika soko la dunia (Price Stabilization Fund) pamoja na kuongeza viwanda vya kuiongezea pamba thamani.

Waziri Mkuu aliwataka wadau wote wa pamba waendelee kushirikiana na Serikali ili kwa pamoja waweze kuinua kipato cha wakulima. “Wadau wa pamba, lazima tuwe na mtazamo wa upeo mpana na wa mbali kuhusiana na mustakabali wa maendeleo ya sekta hii muhimu kwa wananchi wetu na kwa uchumi wa Taifa letu kwa ujumla”, alisema.









All the contents on this site are copyrighted ©.