2013-07-03 09:33:55

Wanawake wakiwezeshwa katika afya, elimu na uchumi, umaskini Barani Afrika utapewa kisogo!


Dhamana ya ukuaji na maendeleo ya Bara la Afrika iko mikononi mwa wanawake wenye madaraka Barani Afrika, ambao wanapaswa kuwa ni wadau wa mabadiliko ya dhati, kwa kuwajengea wanawake wenzao uwezo katika masuala ya elimu, afya na uchumi.

Viongozi wanawake wajisikie kwamba, wanalo jukumu la kusaidia mchakato wa kuleta mabadiliko na maendeleo ya kweli kwa wanawake ili kujenga na kuimarisha taifa kwa leo na kesho yenye matumaini makubwa zaidi. Hii ndiyo changamoto iliyoibuliwa na wake wa Marais zaidi ya kumi kutoka sehemu mbali mbali za Bara la Afrika, katika Kongamano la Kimataifa lililoandaliwa na Taasisi ya George W. Bush wa Marekani, inayopania kuwawezesha wanawake katika masuala ya elimu, afya na uchumi.

Wake hao wa Marais walipata fursa ya kubadilishana uzoefu na vipaumbele katika maisha yao, huku wakichangamotishana kusimama kidete kukabiliana na changamoto pamoja na magumu yanayowasibu watu wao. Kama wake wa Marais wanaweza kutumia ushawishi wao kukoleza maendeleo na kudumisha uhuru na demokrasia Barani Afrika. Huu ni wito ambao umetolewa na Mama Laura Bush, mke wa Rais mstaafu wa Marekani, ambaye amesema atendelea kuunga mkono juhudi za wanawake Barani Afrika katika elimu, afya na uchumi.

Rais Jakaya Kikwete wa Tanzania katika kongamano hilo amewakumbusha wanawake kwamba, wao ni kiungo makini cha mchakato wa maendeleo katika Jamii na Taifa katika ujumla wake. Wanawake ni wadau wakuu wa maendeleo, lakini ndilo kundi kubwa katika Jamii linalokabiliana na umaskini kwani mara nyingi hlifaidi na kile wanachozalisha.

Hii ni changamoto ya kuondokana na mfumo dume ambao umekuwa ni chanzo cha dhuluma na nyanyaso dhidi ya wanawake Barani Afrika. Wanawake wakiwezeshwa katika afya, elimu na uchumi, umaskini Barani Afrika unaweza kupewa kisogo!

Mama Michelle Obama amewataka wake wa Marais kutekeleza majukumu yanayogusa kwanza kabisa mioyo yao, wajitoe kimasomaso kwa ajili ya maendeleo na ustawi wa nchi zao pamoja na kujiwekea mikakati watakayoitekeleza mara baada ya wanaume wao kuondoka madarakani; mwaliko wa kuendelea kuwasaidia wanawake wenzao katika harakati za kujikwamua kiuchumi.

Kongamano hili la siku mbili limehudhuriwa na wake wa Marais kutoka sehemu mbali mbali za Bara la Afrika pamoja na wake wa Mawaziri wakuu na viongozi wa wanawake nchini Tanzania.







All the contents on this site are copyrighted ©.