2013-06-29 10:55:01

Wasi wasi na hofu ya Maaskofu Katoliki Kenya


Baraza la Maaskofu Katoliki nchini Kenya linaendelea kufanya tafakari ya kina kuhusu hali ya maisha ya wananchi wa Kenya kadiri ya uongozi mpya. Maaskofu wanaipongeza Serikali kwa kuleta mabadiliko makubwa mintarafu Katiba Mpya ambayo kimsingi ni sheria mama, kwa kugawa madaraka mikoani, ili kupeleka huduma makini karibu na wananchi, jambo ambalo ni la kwanza katika historia ya Kenya.

Maaskofu Katoliki Kenya wanaonya kwamba, kumeibuka wimbi kubwa la rushwa, ufisadi, upendeleo na uongozi duni; mambo ambayo pengine Serikali kuu haijayafanyia kazi vya kutosha. Kuna baadhi ya viongozi wa kisiasa wametawaliwa mno na ubinafsi kiasi cha kushindwa kuona vipaumbele vya kitaifa, kwa ajili ya mafao ya wengi, maendeleo na ustawi wa wananchi wa Kenya. Kuna baadhi ya mambo kwenye bajeti ya mwaka si ya msingi, lakini yapo kwa ajili ya masilahi ya baadhi ya watu ndani ya Jamii ya Wakenya.

Maaskofu Katoliki wanawataka wananchi wa Kenya kuiwajibisha Serikali yao kwa kuhakikisha kwamba, inatumia vyema rasilimali na mapato ya nchi kwa ajili ya mafao ya wengi. Kanisa kwa upande wake, litaendelea kuwa ni mdau na mshiriki mkuu katika mchakato wa kuwaletea wananchi wa Kenya maendeleo endelevu.

Hii ni changamoto kwa Serikali kuhakikisha kwamba, inaweka miundo mbinu itakayowawezesha wananchi wengi kushiriki katika kupanga, kuamua na kutekeleza maamuzi mbali mbali. Haya yamo kwenye taarifa ya Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya kwa vyombo vya habari, baada ya kuzindua jina jipa la Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya.

Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya linasikitishwa na kinzani na migogoro inayoendelea kujitokeza wakati wa vikao vya Bunge la Kenya na Baraza la Senate. Maaskofu wanayaalika Mabaraza haya mawili kushirikiana katika maboresho ya huduma kwa wananchi wa Kenya badala ya kupimana misuli, jambo ambalo halina tija wala mashiko kwa ustawi na maendeleo ya wananchi wa Kenya.

Maaskofu wanaipongeza Serikali ya Kenya kwa sheria ya elimu ya mwaka 2013 kuhusu elimu ya msingi na kwamba, Kanisa limekuwa ni mdau mkuu katika huduma ya elimu kabla ya uhuru na sasa linaendelea kujitanua kwa viwango na ubora. Maaskofu wanasema, shule zinazomilikiwa na Kanisa zina haki ya kumiliki maeneo yale, ingawa baadhi ya vifungu vinasema kwamba, zimejengwa katika maeneo ya Serikali. Umiliki wa ardhi unaofanywa na taasisi za kidini unapaswa kuheshimiwa kadiri ya Katiba ya nchi.

Maaskofu Katoliki Kenya wanasikitishwa na mfumuko wa bei ya bidhaa na huduma kutokana na ongezeko la thamani kama inavyooneshwa kwenye sheria ya mwaka 2013. Licha ya kuongeza bajeti na makusanyo ya kodi ya Serikali, lakini Serikali inapaswa kutambua kwamba, wananchi wake wengi ni maskini, hawana fursa za ajira na wala hawana kipato cha uhakika! Serikali inawajibu wa kimaadili wa kuhakikisha kwamba, wananchi wanaweza kumudu gharama ya maisha kwa kujipatia mahitaji msingi, yaani: chakula, mavazi na malazi.

Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya linasikitishwa na tofauti kubwa ya nyongeza za mishahara miongoni mwa wafanyakazi wa Serikali na wanataaluma. Malumbano ya mishahara minono yanaweza kulitumbukiza taifa katika maafa makubwa na hivyo Kenya kushindwa kutawalika.

Hii inatokana na ukweli kwamba, walimu wanaendelea na mgomo kwa zaidi ya mara saba, hali ambayo ina dhohofisha sekta ya elimu nchini Kenya na maendeleo ya wanafunzi.

Ni kweli kwamba, walimu wanayo haki ya kufanya mgomo, lakini wanapaswa kutambua kwamba, ualimu ni wito na wanafunzi wana haki ya kusoma. Hapa kuna haja kwa Serikali na walimu kufanya majadiliano ya kina ili kuweza kupata ufumbuzi wa kudumu, anasema Kardinali John Njue, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya.

Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya linahitimisha taarifa yake kwa vyombo vya habari kwa kuwataka waamini kujenga na kuimaarisha moyo wa kimissionari, kwa kuwapenda na kuwathamini jirani, daima wakisukumwa na ari pamoja na moyo wa upendo na mshikamano kwa ajili ya maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii kama walivyofanya Watakatifu Petro na Paulo, miamba ya imani.







All the contents on this site are copyrighted ©.