Mshikamano wa upendo na watoto wagonjwa wanaolazwa kwenye Hospitali ya Bambino Gesù
mjini Roma
Katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Watakatifu Petro na Paulo miamba wa Imani na wasimamizi
wa Mji wa Roma, Jumamosi, tarehe 29 Juni 2013, majira ya jioni kunafanyika maonesho
maalum ambayo kwa Mwaka 2013 yanatolewa kwa ajili ya heshima ya Baba Mtakatifu Francisko
kwa kuchaguliwa kwake kuliongoza Kanisa Katoliki kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.
Lengo ni kukusanya fedha zitakazosaidia kununua vifaa maalum kwa ajili ya
kitengo cha watoto wanaotibiwa kwenye Hospitali ya Bambino Gesù, inayomilikiwa na
kuendeshwa na Vatican. Itakumbukwa kwamba, Hospitali hii imekuwa pia ni msaada mkubwa
kwa watoto wanaotoka katika nchi changa duniani. Hospitali ya Mtakatifu Gaspar, Itigi,
iliyoko, Manyoni, Singida, Tanzania, imekuwa na uhusiano wa karibu zaidi na Hospitali
hii kwa ajili ya huduma kwa watoto wenye magonjwa ya moyo.