2013-06-29 09:30:40

Mshikamano wa upendo na Wananchi wa Amerika ya Kusini


Mfuko wa Maendeleo ya Watu "Populorum Progressio" uliohitimisha mkutano wake wa Mwaka hivi karibuni huko Arequipa, nchini PerĂ¹ na kuhudhuriwa na Kardinali Robert Sarah, Rais wa Baraza la Kipapa linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki, Cor Unum, umekuwa ni kielelezo makini cha alama ya mshikamano wa upendo na wananchi wanaoishi Amerika ya Kusini.

Wajumbe wamechambua na kupitisha miradi mia mbili tu ambayo inapaswa kuwa kweli ni alama ya upendo na mshikamano kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko, kwa ajili ya wananchi wenye asili ya Kiafrika wanaoishi Amerika ya Kusini. Baada ya kufanya upembuzi wa kina anasema Monsinyo Segundo Tejado Munoz, Katibu mkuu mwambata wa Baraza la Kipapa linaloratibu misaada ya Kanisa Katoliki, Cor Unum, miradi 170 tu ndiyo ambayo imeamriwa kwamba, itagharimiwa na mfuko wa Maendeleo ya watu kutokana na kipaumbele na unyeti wake kwa sasa. Hii inatokana na ukweli kwamba, bado athari za myumbo wa uchumi kimataifa zinaonesha makali yake!

Miradi mingi iliyopitishwa inapania kuinua hali ya maisha, ustawi na maendeleo ya wakulima wadogo wadogo, ili waweze kuboresha hali ya maisha yao na kuchangia ustawi wa familia zao katika ujumla wake. Kimsingi hii ni miradi ya: kilimo, afya, elimu na maendeleo endelevu. Lakini, wajumbe kwa mwaka huu wameguswa zaidi na miradi inayoangalia mahangaiko ya ndani ya mwanadamu, yaani miradi inayopania maboresho ya huduma za kichungaji. Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, aliwahi kusema kwamba, watu wanakabiliana na mateso makubwa si tu kwa kukosa vitu bali kwa kutotambua na kuthamini uwepo wa Mungu katika hija ya maisha yao!

Itakumbukwa kwamba, miradi mingi inayohudumiwa na Mfuko wa Maendeleo ya watu inagharimiwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Italia. Kuna haja kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema, kuendelea kuonesha ukarimu zaidi kwa Baba Mtakatifu Francisko ili aweze kuwahudumia watu wengi zaidi wanaohitaji msaada wa hali na mali huko Amerika ya Kusini.

Monsinyo Segundo Tejado Munoz anasema, Mkutano wa Mfuko wa Maendeleo ya Watu kwa ajili ya Amerika ya Kusini, umegusia kwa namna ya pekee, changamoto inayoendelea kutolewa na Baba Mtakatifu Francisko katika kuwahudumia maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Ni kiongozi aliyeonja shida na mahangaiko ya watu wake, ndiyo maana hapo mwakani, wajumbe watafanya mkutano wao wa mwaka mjini Roma, ili waweze kupata nafasi ya kusikiliza changamoto inayotolewa na Baba Mtakatifu Francisko kwa wakati huu.

Mfuko wa Maendeleo ya Watu unaendelea kufanya maboresho katika huduma zake kwa kufanya tafiti kuhusu maisha ya watu mahalia, matatizo, changamoto na fursa zinazopatikana katika maeneo yao, ili kuweza kuwashirikisha kikamilifu katika huduma kwa maskin na hasa wale wanaoishi pembezoni mwa Jamii.

Kuna maendeleo makubwa katika miji, lakini pia maendeleo haya yanaendelea kujenga pengo kati ya maskini na matajiri na kwamba, kuna kundi la watu wengi wanaoishi katika hali ya umaskini wa hali na kipato! Wote hawa wanahitaji kupewa ujumbe wa matumaini kwa wale wanaoishi na wale ambao wako nje ya Kanisa. Upendo na mshikamano vinapaswa kuchukua kasi ya pekee wakati huu watu wanapokabiliwa na athari za myumbo wa uchumi kimataifa! Watu wasikate wala kukatishwa tamaa, waendelee kuwa na matumaini kwa leo na kesho iliyo bora zaidi!







All the contents on this site are copyrighted ©.