Dhamana ya Khalifa wa Mtakatifu Petro ni kuwaimarisha ndugu zake katika imani, upendo
na umoja!
Yesu Kristo amempatia Mtakatifu Petro dhamana ya kuwaimarisha ndugu zake katika imani,
upendo na umoja. Ni maneno ya Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Maadhimisho ya Siku
kuu ya Watakatifu Petro na Paulo miamba wa imani, iliyofanyika kwenye Kanisa kuu la
Mtakatifu Petro mjini Vatican, Jumamosi tarehe 29 Juni 2013.
Katika Ibada
hii ya Misa, Baba Mtakatifu aliwavisha Pallio takatifu, alama ya Kristo mchungaji
mwema, Maaskofu wakuu walioteuliwa hivi karibuni, kutoka katika majimbo makuu thelathini
na matano.
Ibada ya ya misa takatifu, ilitanguliwa na Maaskofu wakuu kula
kiapo cha utii kwa Khalifa wa Mtakatifu Petro na baadaye kuvishwa Pallio takatifu,
alama Uaskofu mkuu na baadaye Ibada ya Misa Takatifu ikaendelea kama kawaida. Katika
mahubiri yake, Baba Mtakatifu amewashukuru Maaskofu kutoka sehemu mbali mbali za dunia
waliofika mjini Vatican kwa ajili ya kuwasherehekea Miamba wa Kanisa, yaani Watakatifu
Petro na Paulo.
Huu ni utajiri mkubwa unaoliwezesha Kanisa kuadhimisha tena
na tena lile tukio la Pentekoste ya kwanza, linalounganisha Familia ya Mungu inayozungumza
lugha mbali mbali katika imani moja! Baba Mtakatifu ametambua uwepo wa ujumbe wa Patriaki
Bartolomeo wa kwanza uliofika mjini Vatican kushiriki katika Maadhimisho ya Siku kuu
ya Watakatifu Petro na Paulo, Miamba wa imani. Nyimbo za Ibada ya Misa zimeongozwa
na Kwaya ya Kanisa la Mtakatifu Tomasi wa Lipsia; jambo ambalo limepamba Ibada hii
na kuonekana kuwa kweli ni ya kiekumene.
Baba Mtakatifu anasema kwamba, Mtakatifu
Petro amepewa dhamana ya kuwaimarisha ndugu zake katika mambo makuu matatu. Hii ni
dhamana aliyokabidhiwa mara tu baada ya kuungama kwamba, Yesu Kristo alikuwa ni Mwana
wa Mungu aliye hai na kwamba, hii ilikuwa ni zawadi ya ufunuo kutoka kwa Baba yake
wa mbinguni. Yesu akampatia dhamana na utume unaobubujika kutokana na imani yake kwa
Kristo Mwana wa Mungu aliye hai.
Baba Mtakatifu anasema, katika Injili, bado
Mitume wa Yesu wameelemewa na mambo ya kidunia, Yesu anapozungumzia kuhusu mateso,
kifo na ufufuko wake, hija ambayo Mwenyezi Mungu amemwandalia kwa ajili ya ukombozi
wa ulimwengu, Mtume Petro anataka kuweka kizingiti! Anafikiri zaidi kuhusu madaraka,
lakini, Yesu anamkanya na kumwambia kwamba, amekuwa ni sehemu ya kikwazo kwake.
Baba
Mtakatifu anaonya kwamba, madaraka katika mwono wa kibinadamu ni hatari katika hija
ya imani na badala yake, waamini wanapaswa kumwachia Mwenyezi Mungu ili aweze kuwakirimia
zawadi ya imani ambayo ni mwanga wa Kristo katika maisha ya Wakristo na utume ndani
ya Kanisa.
Mtakatifu Paulo katika Waraka wake kwa Timotheo anasema kwamba,
amevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo ameumaliza, Imani ameilinda! Baba Mtakatifu
anasema, Mtakatifu Paulo amevipiga vita si kwa kutumia silaha za zilizotengenezwa
kwa mikono ya binadamu ambazo zinaendelea kusababisha maafa makubwa sehemu mbali mbali
za dunia, lakini vita aliyopiga ni maisha ya kifodini!
Silaha kubwa aliyokuwa
nayo mikononi mwake ni Ujumbe wa Yesu Kristo, zawadi kubwa zaidi katika maisha na
utume wake; zawadi ambayo alipenda kuwashirikisha wengine, kiasi kwamba, akajiachilia
mikononi mwa Kristo ili aweze kuyamimina maisha yake bila kujihurumia, ili kujenga
na kuimarisha Kanisa la Kristo. Askofu wa Roma anachangamotishwa na Mama Kanisa kuwaimarisha
ndugu zake katika upendo kwa Kristo, bila ubaguzi wala vikwazo.
Baba Mtakatifu
anasema, Askofu wa Roma amepewa dhamana ya kuwaimarisha ndugu zake katika umoja na
kwamba, Pallio takatifu walizovishwa Maaskofu wakuu ni kielelezo cha umoja na mshikamano
na Khalifa wa Mtakatifu Petro, kielelezo cha umoja na mshikamano katika imani. Uwepo
wa umati mkubwa wa Maaskofu kutoka sehemu mbali mbali za dunia ni kielelezo cha umoja
unaojionesha katika utofauti. Huu ni Urika wa Maaskofu unaoongozwa na Mtakatifu Petro.
Urika huo maadamu umeundwa na wengi, huonesha hali ya Taifa la Mungu ambalo ni la
kiulimwengu.
Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kusema kwamba, ndani ya Kanisa
kuna tofauti kubwa, lakini huu ni utajiri wa Kanisa unaosimikwa katika umoja unaoonesha
Mpango wa Mungu, changamoto ya kuvuka vikwazo na kinzani zinazotaka kuligawa Fumbo
la Mwili wa Kristo, yaani Kanisa. Wote wanapaswa kuungana kwa pamoja, kwani hii ndiyo
ile njia iliyoooneshwa na Yesu mwenyewe! Ikiwa kama Pallio ni alama ya umoja na mshikamano
na Khalifa wa Mtakatifu Petro, pamoja na Kanisa la Kiulimwengu, basi hii pia ni changamoto
ya kila Askofu mkuu kuwa ni chombo cha umoja.
Baba Mtakatifu Francisko, mwishoni
anawaalika waamini kumwachia Mungu mwenyewe nafasi ili aweze kuwafundisha; waweze
kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Kristo na Injili yake, ili kweli waweze kuwa
ni wahudumu wa umoja. Hii ndiyo amana kubwa ambayo waamini wameachiwa na Mitume Petro
na Paulo; amana inayopaswa kumwilishwa na kila Mkristo. Bikira Maria, Malkia wa Mitume
awaombee na kuwasindikiza Maaskofu wakuu katika maisha na utume wao!