Mh. Padre Varghese Thottamkara ateuliwa kuwa ni Askofu mwandamizi wa Jimbo la Kitume
la Nekemte, Ethiopia!
Baba Mtakatifu Francisko amemteua Mheshimiwa Padre Varghese Thottamkara, C.M, kuwa
Askofu Mwandamizi wa Jimbo la Kitume la Nekemte nchini Ethiopia. Askofu mteule alizaliwa
kunako tarehe 2 Juni 1959 huko Thottuva, Jimbo kuu la Ernakulam, India. Mwaka 1982
akajiunga na Shirika la Walazzaro na kuweka nadhiri zake za daima hapo tarehe 10 Mei
1986. Akapadrishwa tarehe 6 Januari 1987.
Tangu wakati huo, amewahi kuwa Paroko,
Gombera na Mwalimu kwenye Seminari kuu ya Shirika iliyoko mjini Addis Ababa, Ethiopia.
Kati ya mwaka 1995 hadi mwaka 1998 alikwenda Roma kujiendeleza kwa masomo na hatimaye
akajipatia Shahada ya Uzalimili katika Taalimungu maadili kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu
Thoma wa Akwino, kilichoko mjini Roma. Kati ya Mwaka 1998 hadi mwaka 2005 alikuwa
ni Mshauri wa Kanda wa Shirika na Jaalim katika Taasisi ya Taalimungu ya Mtakatifu
Francisko iliyoko mjini Addis Ababa.
Kuanzia mwaka 2005 hadi mwaka 2006 alikuwa
ni Mchumi wa Shirika. Mwaka 2006 hadi mwaka 2010 alikuwa ni Mkuu wa Kanda wa Shirika,
Kusini mwa India. Hadi kuteuliwa kwake alikuwa ni Makamu Mkuu wa Shirika.