2013-06-28 08:46:33

Maadhimisho ya Mwaka wa Imani: Imani na matumaini ni chanda na pete!


Kanisa Barani Ulaya, "Ecclesia in Europa" ni Waraka wa kichungaji uliotiwa mkwaju na Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili kunako tarehe 28 Juni 2003. Katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, Makatibu wakuu kutoka Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani Ulaya, kuanzia tarehe 27 Juni hadi tarehe 30 Juni 2013 wanakutana mjini Varsavia, Poland, ili kupembua kwa kina na mapana athari za myumbo wa uchumi kimataifa, ambao umetikisa hata misingi ya imani. Kuna baadhi ya watu wanadhani kwamba, kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, imani tena haina nafasi katika maisha na vipaumbele vyao! Watu wamekata tamaa ya maisha!

Monsinyo Duarte da Cunha, katibu mkuu wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani Ulaya anasema kwamba, imani na matumaini ni chanda na pete na kwamba, Wakristo wanatumwa kutangaza Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia kwa kuwaonjesha wengine ile furaha na imani inayobubujika ndani mwao kutoka kwa Kristo na Kanisa lake. Kristo ni kiini cha Uinjilishaji mpya, dhamana inayofanyiwa kazi na Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya Tatu ya Ukristo.

Athari za myumbo wa uchumi kimataifa ni changamoto kwa waamini kufanya maamuzi machungu juu ya imani yao: kuendelea kumtumainia Kristo au kujishikamanisha na masuala ya uchumi na maendeleo ya teknolojia; mambo ambayo bado hayajaweza kuridhisha ile kiu ya ndani ya mwamini katika hija ya maisha yake hapa duniani? Upendo unaobubujika kutoka kwa Kristo ni mwaliko kwa waamini na watu wote wenye mapenzi mema kuvunja mipaka ya ubinafsi, uchoyo na utaifa, ili kuwaonjesha jirani zao ukarimu na upendo. Bado kuna uwezekano kwa wananchi wa Ulaya kukutana na kuendelea kumtumainia Kristo katika hija ya maisha yao hapa duniani.

Mkutano wa Makatibu wakuu thelathini na watatu kutoka Shirikisho la Maabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani Ulaya, unahudhuriwa na Padre Raymond O' Toole, Katibu mkuu wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani Asia pamoja na Padre Pietro Felet, Katibu mkuu wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu kutoka katika Nchi Takatifu. Wawakilishi hawa wanashirikisha pia hali ya Wakristo kutokana katika nchi zao.







All the contents on this site are copyrighted ©.