2013-06-28 14:19:52

Fumbo la uvumilivu wa Mungu linajionesha katika hija ya maisha ya mwanadamu!


Mwenyezi Mungu anatumia njia mbali mbali ili kuingia kwenye historia ya maisha ya mwanadamu, wakati mwingine anatekeleza mpango wake kwa taratibu, lakini jambo la msingi ni kujenga na kukuza fadhila ya imani na udumifu, bila ya kukata tamaa. Abrahamu alipoambiwa kwamba, angekuwa ni Baba wa Mataifa, alishangaa sana kwani walikuwa wamekwisha kula chumvi ya kutosha na kwa umri wao walikuwa hawategemei tena kupata mtoto!

Katika mazingira kama haya kuna haja kwa waamini kuwa wavumilivu na wadumivu katika maisha ya sala, kwani Mwenyezi Mungu anaendelea kumsubiri binadamu hadi hatima ya maisha yake. Kuna baadhi ya watu walibahatika kukutana na Kristo katika dakika za mwisho wa maisha yao!

Yule mwizi aliyekuwa ametundikwa Msalabani pamoja na Yesu pale Mlimani Kalvari, alimgundua Mwenyezi Mungu katika dakika za mwisho mwisho wa maisha yake. Hivi ndivyo ilivyotokea kwa wale Wanafunzi wa Emmaus. Wakati mwingine mwamini anasahau kwamba, Mwenyezi Mungu anafanya hija pamoja naye katika maisha, hata pale wanaposahau, bado Mwenyezi Mungu anaonesha uvumilivu mkuu.

Hii ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae Marthae, kilichoko mjini Vatican, siku ya Ijumaa, tarehe 28 Juni 2013. Baba Mtakatifu amewatafakarisha haya viongozi waandamizi na wafanyakazi kutoka Idara ya Afya ya Vatican kuhusu Fumbo la uvumilivu wa Mwenyezi Mungu katika hija ya maisha ya mwanadamu.

Kuna wakati ambapo mwamini anakumbana na giza pamoja na utupu katika maisha yake ya kiimani, hapo ndipo anapotamani kushuka kutoka kwenye Msalaba, kwani amekosa uvumilivu! Haya ndiyo waliyokuwa wanamwambia Yesu alipokuwa pale juu ya Msalaba, lakini aliwaonesha uvumilivu wa ajabu hadi chembe ya mwisho ya maisha yake, alipoinamisha kichwa, akakata roho!

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini kumwomba Mwenyezi Mungu neema ili aweze kufanya hija ya maisha pamoja nao, kama inavyojionesha katika maisha ya Abraham bila ya kukata tamaa!







All the contents on this site are copyrighted ©.