2013-06-26 15:04:30

Waislam na Wakristo wanayo dhamana ya kulinda na kutetea maisha ya kiroho, maadili na utu wema!


Tume ya pamoja kati ya waamini wa dini ya Kiislam na Kikatoliki, hivi karibuni, imehitimisha mkutano wake wa mwaka uliokuwa chini ya uongozi wa Kardinali Jean Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini. Katika mkutano huu, ujumbe kutoka kwa waamini wa dini ya Kiislam uliongozwa na Professa Hamid Bin Ahmad Al Rifaie, Rais wa Jukwaa la Kimataifa la dini ya Kiislam kwa ajili ya majadiliano ya kidini.

Katika majadiliano yao ya pamoja, wametambua na kuridhia umuhimu wa mambo ya kiroho na maisha ya kidunia, wajibu kwa waamini wa dini hizi mbili ni kuhakikisha kwamba, wanajitahidi kuweka uwiano mzuri katika masuala haya mintarafu mwelekeo wa maisha. Watu wengi duniani wanakabiliana na mmong'onyoko wa tunu msingi za maisha ya kiroho na kimaadili, mwaliko kwa waamini wa dini hizi mbili kuwalinda na kuwatetea wanyonge katika hali kama hizi kwa kukazia maadili na utu wema.

Wajumbe hawa wamekubaliana kimsingi kwamba, leo hii kuna aina nyingi za kinzani na migogoro, wajibu wao kama waamini ni kuwalinda watu wanaokabiliwa na hali kama hizi. Wajumbe hawa wanasema walipata nafasi ya kuweza kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko, aliyewahimiza kuendeleza dhamana hii nyeti kwa kuheshimiana na kuthaminiana ili majadiliano miongoni mwa waamini wa dini hizi mbili yaweze kuzaa matunda ya amani, ustawi na maendeleo endelevu.

Wajumbe katika ujumla wao, wamelaani vita inayoendelea nchini Syria na hivyo kupelekea mauaji ya watu wasiokuwa na hatia, jambo ambalo ni kinyume kabisa cha utakatifu wa maisha ya binadamu. Wajumbe wanapenda kutoa mwaliko kwa viongozi wa Jumuiya ya Kimataifa kuongeza juhudi zaidi ili kuweza kupata suluhu ya mgogoro wa Syria na hivyo kusitisha mauaji ya watu wasiokuwa na hatia.

Wajumbe wa Tume hii ya pamoja, wamekubaliana kwamba, watakutana tena kwa mkutano mwingine, utakaofanyika mjini Tatwan, Morocco, lakini utatanguliwa na maandalizi na kwamba, mkutano huu utaandaliwa na upande wa waamini wa dini ya Kiislam.







All the contents on this site are copyrighted ©.