2013-06-26 07:53:33

Mkusanyiko wa Katekesi za Baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto XVI ni utajiri mkubwa katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani


Idara ya Uchapaji ya Vatican imechapisha kitabu ambacho ni mkusanyiko wa Katekesi za Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, tangu tarehe 10 Oktoba 2012 hadi tarehe 27 Februari 2013 siku moja kabla ya kung’atuka kutoka madarakani kama Khalifa wa Mtakatifu Petro ili kupata nafasi ya kupanda kwenda Mlimani kwa ajili ya kutafakari na kusali kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo. RealAudioMP3

Kitabu hiki cha Mkusanyiko wa Katekesi za Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, kina utajiri mkubwa wa sanaa zinazoonesha Kanuni ya Imani katika michoro maarufu. Huu ni utajiri unaonesha kwa namna ya pekee Maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, ambalo limekuwa ni tukio kubwa katika maisha na utume wa Kanisa katika Mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.

Mwaka wa Imani ni mwaliko kwa Waamini kuwa na ari na mwamko mpya katika: kuifahamu, kuiadhimisha, kuimwilisha katika maisha adili pamoja na kuisali kama sehemu ya mchakato wa ushuhuda wa imani tendaji. Ni changamoto ya kuendelea kumtangaza Yesu Kristo kuwa kweli ni Mkombozi wa Ulimwengu kwa njia ya ushuhuda wa maisha unaoonesha umuhimu wa imani kwa Kristo na Kanisa lake. Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, katika katekesi zake kwa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani amejaribu kujibu swali la msingi imani ni kitu gani kwa mwamini katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia?

Ameangalia umuhimu wa imani inayoungamwa na Jumuiya ya Wakristo; kiu ya kumfahamu Mwenyezi Mungu na hamu ya kutaka kumpeleka katika moyo wa mwanadamu! Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, katika Katekesi zake anajaribu kumwonesha mwamini jinsi anavyoweza kumfahamu mwenyezi Mungu, maana ya ufunuo unaojionesha kwa namna ya pekee katika upendo unaojikita katika Fumbo la Utatu Mtakatifu.

Anaonesha nafasi ya Bikira Maria katika imani, kwa kuanzia katika Fumbo la Umwilisho, Bikira Maria ni Mama aliyeonesha utii wa imani. Nafasi ya Roho Mtakatifu, Kanuni ya Imani ni mambo ambayo mwamini anapaswa kuyafahamu kwa kina kama sehemu ya hija yake ya imani hapa duniani.

Baba Mtakatifu amegusia pia vishawishi ambavyo Yesu alikutana navyo alipokuwa Jangwani. Kwa hakika, Mwaka wa Imani unapania kuwaimarisha waamini katika imani yao kwa Fumbo la Utatu Mtakatifu, Kanisa na Mambo ya nyakati. Kila mtu anapaswa kutambua na kuonja kwamba, anapendwa na kuthaminiwa na Mwenyezi Mungu ndiyo maana akamtuma Mwanaye wa Pekee yesu Kristo aweze kuja ulimwenguni, akabiliane na mateso, kifo na hatimaye, siku ya tatu kufufuka kutoka katika wafu ili kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi mauti.

Ni changamoto kwa kila Mkristo kusikia ile furaha ya kuwa kweli ni mfuasi wa Kristo ili hatimaye, aweze kuitolea ushuhuda wa kweli katika uhalisia wa maisha.

Imani ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu na hakuna mtu anayeweza kuipokonya, lakini inapaswa kurutubishwa kwa: sala, tafakari ya Neno la Mungu, Sakramenti za Kanisa na Matendo ya Huruma yanayoonesha imani katika matendo.








All the contents on this site are copyrighted ©.