2013-06-25 07:26:06

Ulimwengu unahitaji kuona ushuhuda wa pamoja unaotolewa na waamini wa dini mbali mbali katika kulinda, utu, heshima, haki na amani duniani!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu tarehe 24 Juni 2013 amekutana na kuzungumza na ujumbe wa Tume ya Wayahudi ya Majadiliano ya Kidini Kimataifa, uliomtembelea mjini Vatican. Kwa takribani miaka arobaini, Kanisa Katoliki limekuwa likifanya majadiliano ya kidini na Wayahudi, hali ambayo imechangia kuimarika kwa urafiki kati ya waamini wa dini hizi mbili.

Tume hii inatarajiwa kufanya tena mkutano wake mwezi Oktoba, 2013 mjini Madrid, Hispania kwa kuongozwa na kauli mbiu "Changamoto za kiimani katika Jamii mamboleo". Baba Mtakatifu Francisko anasema, tangu aanze kutekeleza utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro amebahatika kukutana na kuzungumza na viongozi mbali mbali wa dini ya Kiyahudi, lakini kwa mara ya kwanza amezungumza rasmi na Tume hii.

Kwa upande wa Kanisa Katoliki, Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican umekuwa ni msingi rejea wa majadiliano ya kidini na kwa namna ya pekee na waamini wa dini ya Kiyahudi kwamba, kuna cheche za imani kutoka kwa Mababu na Manabii wanazoshirikishana. Baba Mtakatifu amelaani vitendo vya chuki, madhulumu na ubaguzi unaofanywa kwa misingi ya kidini na kusema kwamba, mizizi ya imani ya dini hizi mbili haiwezi kuruhusu msimamo kama huu!

Misingi mikuu ya imani iliyobainishwa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican imekuwa ni dira na kielelezo cha majadiliano baina ya waamini wa dini hizi kama sehemu ya mchakato wa kufahamiana na kuthaminiana, hali ambayo imejionesha kwa namna ya pekee katika kipindi cha miaka kumi iliyopita. Kumekuwepo na nyaraka mbali mbali zinazobainisha misingi ya uhusiano wa kitaalimungu kati ya Wayahudi na Wakristo, jambo ambalo waamini wanapaswa kumshukuru Mungu.

Baba Mtakatifu anasema kwamba, majadiliano ya kidini na Wayahudi ni jambo ambalo linaendelea kuota mizizi yake hata katika Makanisa mahalia, kama alivyojitahidi kutekeleza wakati alipokuwa Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Buenos Aires. Alipata nafasi ya kujadiliana kwa kina na mapana kuhusu utambulisho wao wa kidini, sura ya binadamu mintarafu Maandiko Matakatifu; jinsi ya kuuhisha uwepo wa Mungu kati ya walimwengu waliokengeuka na pamoja na jinsi ambavyo waamini wa dini hizi mbili wanavyoweza kupambana na changamoto za kiimani.

Jambo kubwa zaidi anasema Baba Mtakatifu ni ile hali ya kuthamini uwepo wao, majadiliano, ukarimu na kusaidiana kwa hali na mali kama waamini. Urafiki kati ya watu ni msingi thabiti wa majadiliano ya kidini, changamoto ya kuwahusisha vijana wa kizazi kipya. Ulimwengu unahitaji kuona ushuhuda wa pamoja unaotolewa na waamini wa dini mbali mbali duniani katika kulinda, kudumisha na kutetea utu na heshima ya binadamu, haki na amani ambayo kimsingi ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu.







All the contents on this site are copyrighted ©.