2013-06-25 15:12:01

Maadhimisho ya Mwaka wa Imani: Siku ya Familia: 26 hadi 27 Oktoba 2013


Baraza la Kipapa la Familia limeanza kuandikisha majina ya familia ambazo zinapenda kushiriki katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, kwa kutembelea Kaburi la Mtakatifu Petro katika kilelle cha Maadhimisho haya kwa Familia hapo tarehe 26 hadi 27 Oktoba 2013 hapa mjini Vatican. Maadhimisho haya yanaongozwa na kauli mbiu "Familia inaishi furaha ya imani!

Hii itakuwa ni fursa makini kwa Familia kutoka sehemu mbali mbali za dunia kuweza kukutana pamoja kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro ili kusali, kutafakari na kushirikishana furaha ya imani inayobubujika kutoka kwa Yesu Kristo Mkombozi wa dunia. Ni muda wa kutolea ushuhuda wa nguvu tunu msingi za maisha ya kifamilia na utu wema. Wanafamilia watapata nafasi nyingine tena ya kugundua umuhimu wa Familia kama mahali muafaka pa kurithisha imani ya Kikristo.

Katika Maadhimisho haya, watoto wenye umri kati ya miaka 3 hadi 12 wanaalikwa kutuma michoroinayohusiana na Familia zao; michoro ambayo itawasilishwa kwa Baba Mtakatifu Francisko, ili kujionea ufahamu wa watoto kuhusiana na Familia zao. Watoto wenye umri kati ya miaka 13 hadi 18 wataweza kuwashirikisha wengine picha za familia zao kwa kutuma kwenye mtandao wa Baraza la Kipapa la Familia. Vijana wenye karama na vipaji mbali mbali watashiriki pia katika tamasha linaloonesha karama na vipaji vya familia.

Ratiba elekezi kwa ajili ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani kwa Familia inaonesha kwamba, tarehe 26 Oktoba, Familia kutoka sehemu mbali mbali za dunia zitapata nafasi ya kuungama ili kuweza kupokea rehema na neema zinazotolewa na Mama Kanisa katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani. Mchana Familia hizi zitakutanika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro. Jioni, Familia zitasali kwa pamoja na baadaye zitaungana na Baba Mtakatifu Francisko ili kukiri imani kwa pamoja.

Kilele cha Maadhimisho haya ni hapo Jumapili, tarehe 27 Oktoba. Saa 3: 30, Familia zitasali na kutafakari kwa pamoja Rozari Takatifu; muhtasari wa Injili na baadaye zitajiunga na Baba Mtakatifu kwa ajili ya Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu, inayotarajiwa kuongozwa na Baba Mtakatifu Francisko pamoja na kusali kwa pamoja Sala ya Malaika wa Bwana.







All the contents on this site are copyrighted ©.