2013-06-21 07:47:18

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 12 ya Kipindi cha Mwaka C wa Kanisa


Ninakuleteeni ujumbe wa Neno la Mungu katika Dominika ya 12 ya Mwaka C. Mama Kanisa ametuwekea Neno litupalo wajibu wa kutambua yakwamba mfuasi wa Bwana si yule anayefahamu mambo bali yule anayeishi mafundisho ya Bwana, anayejitwika msalaba wake kila siku na kumfuasa Bwana. RealAudioMP3

Katika Injili ya Luka 9:18-24 ambayo tunaitafakari Bwana yuko faragha anasali, na wanafunzi wako pamoja naye. Katika kusali anawauliza wanafunzi wake, hivi watu wanasema mimi ni nani? Na ninyi mwasema mimi ni nani? Kwa hakika anawauliza wanafunzi juu ya asili yake, anataka wanafunzi wake wawe na uhakika wa yule wanayemfuata ni nani na lengo la maisha yake ni nini!

Swali la kwanza ni kwa ajili ya kutambua watu wanasema nini na swali la pili anataka sasa kundi la Mitume hawa katika uhalisia wao waweze kutoa jibu ambalo litakuwa kielelezo cha mwelekeo wa kazi yao ya kichungaji mara wanapomaliza malezi yao katika seminari ya Kristo.

Mara moja atufundisha kuishi uhalisia kamili wa mambo, anataka kila mmoja wetu aingie katika mahusiano ya moja kwa moja naye na wala si katika makutano. Anataka kila mmoja aingie katika mtima wa dhamiri yake na kuweza kugundua Bwana ni nani. Anapowauliza atatumia kiwakilishi “ninyi” mwasema mimi ni nani badala ya “wewe”, katika hili pengine anaona mmoja anaweza kuingia katika woga na hivi Bwana anataka jibu ambalo linasimikwa katika maisha ya Jumuiya, ndiyo kusema Kanisa.

Baada ya maswali hayo na hasa swali msingi yaani swali la pili linakuja jibu halisia toka kwa Mtume Petro akisema “wewe ndiye Kristo wa Mungu” na kisha Bwana anawaonya wasimwambie mtu yeyote. Katika jibu tunatambua kuwa kumbe Bwana ni mpakwa mafuta wa Bwana atokaye kwa Mungu, kuhani milele anayetuletea zawadi za kimungu toka mbinguni. Inaonekana pia alama ya ukuu wa Mt. Petro katikati ya kundi la Mitume.

Mara baada ya jibu la Mitume Bwana atasonga mbele na kutoa sasa kiini cha mafundisho yake yaani mateso hadi ufufuko wake ambapo sasa kuna madai makubwa si kumfahamu tu bali sasa kushika msalaba na kumfuata kila siku. Wanafunzi wanaposikia mateso haya wataogopa na ndiyo maana hapo mwanzoni aliwaambia wasimwambie mtu. Anatangaza siri ya kimasiha.

Bwana anataka wanafunzi wake wamfuate kikwelikweli kama ambavyo alivyo waita mwanzoni alisema nifuate na kumfuata ndo huko kunakotupeleka mpaka msalabani. Katika kumfuata kuna kupoteza maisha lakini ndiko kuna maisha, yaani maisha kweli maisha ya milele.

Mpendwa mwana wa Mungu maisha yetu katika imani yanadai kusimama kidete na kufuata njia ya Kalivari pamoja na Kristo. Ni maisha ya kujitoa sadaka kwa ajili ya Kanisa na kwa ajili ya wote, ni kumwombolezea yule waliyemchoma na kwa njia ya majitoleo yako basi neema na zawadi mbalimbali za kimungu zinashuka toka juu.

Ni kujitahidi daima kujenga umoja wa Kanisa ambao tulipewa kwa njia ya ubatizo kama ambavyo Mtakatifu Paulo anawaambia Wagalatia akisema: kwa njia ya Ubatizo wote tumefanywa kuwa sawa. Hakuna tena Myahudi wala Myunani na hapana mtumwa wala mtu huru.

Basi kila mmoja ni mrithi wa ahadi za Mungu alizotuhaidia kwa njia ya Ibrahimu. Kumbe sasa msalaba wako ni kujenga usalama na amani katika taifa la Mungu. Nikutakie Dominika njema na tukutane tena Juma lijalo wasaa na wakati kama huu. Tumsifu Yesu Kristo.

Tafakari hii imeletwa kwako na Pd Richard Tiganya C.PP.S









All the contents on this site are copyrighted ©.