“Kuondoa Mila Zenye Kuleta Madhara kwa Watoto: Ni Jukumu Letu Sote”
Ifuatayo ni hotuba ya Mheshimiwa Sophia M. Simba, Waziri maendeleo ya Jamii, Jinsia
na Watoto nchini Tanzania alipokutana na waandhisi wa habari kuhusu maadhimisho ya
Siku ya Mtoto wa Afrika yaliyofikia kilele chake tarehe 16 Juni 2013.
Ndugu
Waandishi wa Habari,
Tarehe 16 Juni, 2013 ni kilele cha maadhimisho ya Siku
ya Mtoto wa Afrika. Siku hii huadhimishwa na nchi zote wanachama wa Umoja wa Afrika
kwa mujibu wa Azimio lililopitishwa na nchi 51 za Umoja huo mwaka 1990. Azimio hili
lilipitishwa kwa ajili ya kukumbuka mauaji ya watoto wa shule yaliyofanyika katika
kitongoji cha Soweto, Afrika ya Kusini tarehe 16 Juni 1976. Kama tunavyofahamu siku
kama hiyo watoto wapatao 2,000 waliuwawa kikatili na iliyokuwa Serikali ya Makaburu
wakati wakiwa kwenye harakati za kudai haki yao ya msingi ya kutokubaguliwa kutokana
na rangi yao. Kwetu sisi Watanzania siku hii ni muhimu sana kwa vile inazingatia maslahi
ya watoto. Inatukumbusha sisi wazazi, walezi, taasisi/mashirika na Serikali kwa ujumla
kuhusu wajibu na majukumu yetu kwa watoto.
Lengo na madhumuni:
Tanzania
kama mwanachama wa Umoja wa Afrika, imekuwa ikishiriki kikamilifu kuadhimisha siku
hii kwa miaka ishirini na mbili mfululizo tangu mwaka 1991. Lengo la maadhimisho haya
ni kuelimisha wananchi kuhusu haki, ustawi na maendeleo ya watoto wa jinsi zote. Kwa
upande wao, watoto wanapata nafasi maalum ya kujieleza, kusikilizwa, kushiriki na
kuonyesha vipaji vyao katika hatua za kujiendeleza wakati wa maadhimisho haya. Kwa
ujumla madhumuni ya maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika ni pamoja na:-
·Kuinua
kiwango cha uelewa na ufahamu wa matatizo yanayowakabili watoto wa Afrika ·Kukumbusha
na kuhamasisha jamii kuhusu utoaji wa haki za msingi za watoto. ·Kuwaendeleza watoto
kielimu, kiafya, kiutamaduni na kimaadili na kuhakikisha ustawi wa watoto wote bila
ubaguzi wa aina yoyote.
Aidha, Serikali kwa kupitia Wizara ya Maendeleo ya
Jamii, Jinsia na Watoto hutumia siku hii:- ·Kutathmini kwa kina utekelezaji wa
Sera ya Maendeleo ya Mtoto, Sera nyingine za kisekta zinazohusu watoto, Sheria ya
Mtoto Na.21/2009 pamoja na mikataba ya kimataifa na kikanda kuhusu haki na ustawi
wa Mtoto. ·Kuhakikisha watoto wanapata nafasi ya kujieleza na kusikilizwa katika
masuala yanayohusu maendeleo na ustawi wao, kwa kupitia fursa tulizo nazo ikiwa ni
pamoja na kutumia vyombo vya habari vya taifa. ·Kuhimiza kuwekeza rasilimali za
kutosha katika afya, elimu na lishe bora ya watoto kama haki zao za msingi.
Kaulimbiu Katika
kuadhimisha maadhimisho haya tumekuwa na kawaida ya kuandaa kaulimbiu ambayo kwa namna
moja ama nyingine inalenga kuihamasisha jamii kuhusu changamoto mbalimbali zinazowakumba
watoto nchini na Afrika kwa ujumla. Mfano kaulimbiu ya mwaka 2011 ilikuwa ni “Tuungane
kwa Pamoja Kuchukua Hatua za Haraka Kushughulikia Tatizo la Watoto Wanaoishi Mitaani(All
Together for Urgent Actions in Favour of Street Children)”, kaulimbiu ya mwaka 2012
ilikuwa ni “Haki za Watoto Wenye Ulemavu: Ni Wajibu Wetu Kuzilinda, Kuziheshimu, Kuziendeleza
na Kuzitimiza (The Rights of Children With Disabilities: The Duty to Protect, Respect,Promote
and Fulfill)”.
Hivyo basi, kaulimbiu ya mwaka 2013 inasema “Kuondoa Mila Zenye
Kuleta Madhara kwa Watoto: Ni Jukumu Letu Sote” (Eliminating Harmful Social and Cultural
Practices: Our Collective Responsibility). Lengo la kaulimbiu hii ni kuihamasisha
jamii yetu kubaini baadhi ya mila ambazo zimekuwa zikipelekea madhara mbalimbali kwa
watoto wetu iwe ni kimwili na hata kisaikolojia. Kuendelea na mila hizi kunakinzana
na utekelezaji wa Sera ya Maendeleo ya Mtoto (2008), Sheria ya Mtoto Na. 21/ 2009
na mikataba ya kimataifa na kikanda kuhusu haki na ustawi wa watoto ambayo nchi iliiridhia.
Ndugu Waandishi wa Habari Nchi yetu ina makabila mbalimbali ambapo kila
kabila lina mila na tamaduni zake. Mila hizi kwa kiasi kikubwa zimekuwa zikisaidia
kuleta amani na uelewano katika jamii zetu, lakini vile vile mtakubaliana nami kuwa
kuna baadhi ya mila zimeleta changamoto kubwa katika kumtimizia mtoto haki zake za
msingi. Haki hizi ni pamoja na haki ya kuishi, kulindwa, kuendelezwa, kushiriki na
kutokubaguliwa.
Naomba nitoe mfano wa tatizo la ukeketaji kwa watoto wa kike
linalofanywa na baadhi ya makabila hapa nchini. Kitendo hiki kinakinzana na haki nilizozitaja
hapo juu kwa kiasi kikubwa hasa ukichukulia namna zoezi zima la ukeketaji linavyofanyika
na mazingira yake ambapo mtoto anawekwa katika mazingira mepesi ya kupata maambukizi
ya virusi vya ukimwi na hatimaye kuathirika na UKIMWI. Lakini pia zoezi hili humuathiri
sana mtoto kisaikolojia kutokana na namna linavyoendeshwa. Hivyo basi, pamoja na kutambua
umuhimu wa mila zetu hapa nchini, kuna haja sasa ya kuzifanyia tathmini ya mchango
wake katika suala la malezi, makuzi na maendeleo ya awali na ya baadaye kwa watoto
wetu.
Ndugu Waandishi wa Habari, Napenda kuchukua fursa hii pia kuwataarifu
kuwa maadhimisho haya kwa mwaka huu yataadhimishwa katika ngazi ya Mkoa ambapo kila
mkoa utaaadhimisha siku hii kwa kushirikisha na Halmashauri za wilaya/Manispaa/Miji,
kata, vijiji, mashirika na taasisi mbalimbali zilizoko katika Mkoa husika na watu
binafsi. Hii itaipa mikoa nafasi nzuri ya kutafakari matatizo yanayowakabili watoto
ikiwa ni pamoja na kuwapatia haki zao za msingi. Mikoa itapata pia nafasi ya kuweka
miradi endelevu kwa ajili ya kuwandeleza watoto.
Mwisho Ndugu zangu wanahabari
nawashukuru kwa ushirikiano wa hali ya juu kama mnavyofanya mara nyingi katika kuihamasisha
jamii yetu kuhusu masuala ya watoto na maendeleo yao. Napenda kuwapongeza na kuwashukuru
sana kwa kushirikiana na Wizara yangu katika kuijenga “Tanzania Imfaayo Mtoto”. Ni
matumaini yangu pia mtaendelea kuwa chanzo kizuri cha kufichua vitendo vya ukatili
wanavyofanyiwa watoto kama ambavyo mmekuwa mkifanya kwa muda mrefu sasa.
Baada
ya kusema haya, naomba niwatakie wananchi wote maadhimisho mema ya siku hii na kila
mmoja wetu aangalie ni vipi anashiriki kumpatia mtoto wake na watoto wote wa Tanzania
haki zao. Hili ni jukumu letu sote.
Asanteni sana kwa kunisikiliza na nawatakia
kazi njema