2013-06-15 08:15:42

Wajumbe wa Vietnam na Vatican waliridhishwa na mchakato wa uhusiano kati ya nchi hizi mbili!


Mkutano wa nne wa kikosi kazi cha ushirikiano kati ya Vatican na Vietnam umehitimishwa hivi karibuni mjini Vatican. Ujumbe wa Vietnam kwenye mkutano huu uliongozwa na Bwana Bui Thanh Son, Naibu Waziri wa mambo ya nchi za nje na ujumbe wa Vatican uliongozwa na Monsinyo Antoine Camilleri, Katibu mkuu msaidizi wa mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican.

Wajumbe pamoja na mambo mengine wamepembua uhusiano kati ya Vatican na Vietnam pamoja na Kanisa Katoliki nchini humo katika ujumla wake. Vatican imeishauri Serikali ya Vietnam kuendelea kuboresha uhuru wa kuabudu pamoja na kutoa nafasi kwa dini kuchangia ustawi na maendeleo ya nchi yao kiuchumi na kijamii. Vatican imeishukuru Serikali ya Vietnam kwa mchango wake mkubwa katika kufanikisha Maadhimisho ya Mkutano mkuu wa kumi wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Asia uliofanyika nchini humo kunako Mwezi Desemba 2012.

Vatican pia imeishukuru Serikali kwa ushirikiano mwema wakati wa ziara ya kikazi iliyofanywa na Askofu mkuu Leopoldo Girelli nchini humo na kwamba, imeonesha utashi wa kuanzisha uhusiano wa kidiplomasia na Vietnam kwa kuwa na mwakilishi wa Vatican nchini humo kwa ajili ya mafao ya pande hizi mbili.

Ujumbe wa Vatican umesema kwamba, Kanisa litaendelea kuchangia kwa hali na mali ustawi na maendeleo ya nchi ya Vietnam, kwa kumwilisha Injili sanjari na waamini wake kuendelea kuwa ni raia wema. Kanisa litaendelea pia kutoa Mafundisho yake Jamii kwa wananchi wa Vietnam.

Pande hizi mbili zinaridhishwa na uhusiano ambao umekuwepo kati yao, kwa kuendelea kushirikiana vyema pamoja na kubadilishana misingi ya uhusiano wa kidiplomasia na kwamba, wataendelea kujenga uhusiano zaidi kwa kuwezesha kuwa na Balozi wa Vatican nchini Vietnam asiyemkazi, ili kumwezesha kutekeleza majukumu yake kwa ukamilifu zaidi.

Mkutano wa awamu ya tano unatarajiwa kufanyika mjini Ha Noi, nchini Vietnam na kwamba, mkutano huu utapangwa kufuatia mazungumzo ya kidiplomasia. Wajumbe kutoka Vatican walipata nafasi ya kukutana na kuzungumza na Askofu mkuu Dominique Mamberti, Katibu mkuu wa Mambo ya nchi za nje na ushirikiano wa Kimataifa mjini Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.