Waamini wanachangamotishwa kuwa ni wadau wa huduma ya mapendo kwa jirani zao kama
njia ya kukoleza misingi ya amani!
Kanisa Katoliki linaendelea kushirikiana na waamini wa dini mbali mbali kwa ajili
ya kuombea na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano kwa ajili ya
mafao ya wengi na ustawi wa binadamu mahali popote pale alipo. Huduma na amani ni
chanda na pete katika maisha ya waamini. Ni changamoto iliyotolewa na Kardinali Jean
Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini wakati wa sala ya
pamoja kwa ajili ya kuombea amani iliyofanyika kwenye Ukumbi wa Kanisa kuu la Westminster,
Jumamosi tarehe 15 Juni 2013.
Itakumbukwa kwamba, Kardinali Tauran yuko nchini
Uingereza kwa ziara maalum ya kikazi inayopania pamoja na mambo mengine kujenga na
kuimarisha urafiki urafiki miongoni mwa waamini wa dini mbali mbali ili kwa pamoja
waweze kusimama kidete kulinda na kutetea amani, changamoto kutoka kwa Baba Mtakatifu
mstaafu Benedikto wa kumi na sita, ambayo inaendelea kufanyiwa kazi kwa sasa.
Umoja,
upendo na mshikamano miongoni mwa waamini wa dini mbali mbali ni nyenzo msingi katika
kujenga na kudumisha amani. Katika ziara yake nchini Uingereza, Kardinali Tauran amekutana
na waamini wa dini ya Kihindu, Kijanisti na siku ya Jumamosi, amekutana na waamini
wa dini la Kisikh, wanaohamasishwa kushirikiana ili kujenga misingi ya haki na amani.
Ni mwaliko kwa waamini wa dini hizi mbili kufahamu kwamba, kuna furaha kubwa kwa waamini
kutolea muda, vipaji, karama na nguvu zao kwa ajili ya mafao na furaha ya wengine.
Kardinali
Tauran anasema kwamba, ulimwengu mamboleo umesheheni tabia ya watu kutaka kumezwa
zaidi na malimwengu, hali inayoonesha ulaji wa kutupwa, mmong'onyoko wa kimaadili
na utu wema; ubinafsi, tamaa na uchu wa mali na madaraka; mambo ambayo kwa namna moja
au nyingine yanachangia kinzani na migogoro ya kisiasa, kijamii na kiuchumi na pengo
kubwa kati ya maskini na matajiri; na umati wa watu unaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.
Waamini
wanaweza kuchangia katika mchakato wa kuleta ugawanaji sawa wa rasilimali, mapato
na utajrii wa nchi pamoja na fursa mbali mbali zinazojitokeza kwa ajili ya ustawi
na maendeleo ya nchi husika. Kwa pamoja wasimame kidete kupinga vitendo vya rushwa,
wizi, ufisadi na ubadhirifu wa mali ya umma; daima wakijitahidi kujenga na kudumisha
Jamii inayosimikwa katika misingi ya haki, amani na usawa kwa ajili ya mafao ya wengi.
Kardinali Tauran anasema kwamba, kuna uhusiano mkubwa wa uelewa wa huduma
kama kielelezo cha upendo kwa Mungu na jirani, hali inayojionesha kwa namna ya pekee
kutoka kwa Kristo aliyewaambia mitume wake kwamba, hakuja ulimwenguni ili kuhudumiwa
bali kuhudumia na kutoa maisha yake ili yaweze kuwa ni fidia ya wengi.
Waamini
wa dini hizi mbili wanaweza kutolea ushuhuda kama mtu binafasi au kama Jumuiya kwa
njia ya huduma inayomwilishwa katika matendo. Huduma hii itolewe kwa maskini na wote
wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii, kwa njia ya majadiliano ya kidini na ujenzi wa
amani, daima wakijitahidi kuendeleza mchakato wa kutafuta ukweli na amani ya kudumu.