2013-06-15 14:20:36

Tafuteni mafao ya wengi; dumisheni utu na heshima ya binadamu!


Baba Mtakatifu Francisko, Jumamosi, tarehe 15 Juni 2013 amekutana na kuzungumza na Wabunge kutoka Ufaransa wanaowakilisha sera na maoni tofauti, lakini kwa pamoja wameonesha uhusiano mwema uliopo kati ya Vatican na Ufaransa. Anasema, anapenda kukazia dhamana na wajibu walio nao wabunge na Kanisa katika maisha ya hadhara.

Baba Mtakatifu anatambua kwamba, Serikali ya Ufaransa haina dini na kwamba, uhusiano wake na dini pamoja na madhehebu mbali mbali nchini humo hauna haja ya kuwa na misigano inayopelekea hata dini na mashirika yake kutohusishwa kikamilifu katika ujenzi, ustawi na maendeleo ya wananchi wa Ufaransa. Kwa pamoja wanaweza kusimama kidete kulinda na kudumisha utu na heshima ya binadamu pamoja na kutafuta mafao ya wengi mambo ambayo ni sehemu ya Mafundisho Jamii ya Kanisa. Kanisa linapenda kuchangia katika ustawi na maendeleo ya wananchi wa Ufaransa katika medani mbali mbali za maisha.

Kama wawakilishi wa wananchi waliowachagua katika ngazi ya kitaifa, Wabunge wanahamasishwa kushiriki kikamilifu katika maboresho ya maisha ya wapiga kura wao kwa kuguswa na mahitaji yao msingi. Kama wabunge, wanatekeleza majukumu yao mintarafu sheria ambazo zinapaswa pia kusaidia mchakato wa maboresho ya maisha ya mwanadamu.

Baba Mtakatifu Francisko, mwishoni anawatakia kila la kheri na baraka tele katika utume wao kwa wananchi wa Ufaransa, daima wakitafuta mafao ya wengi sanjari na kudumisha umoja na udugu miongoni mwao!







All the contents on this site are copyrighted ©.