2013-06-15 10:23:46

Jeshi la Polisi kushirikiana na viongozi wa Kanisa kupambana na uhalifu ndani ya Jamii


Kardinali Polycarp Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, hivi karibuni alikutana na kuzungumza na Mkuu wa Jeshi la Polisi Insipekta Jenerali Said Mwema. Kardinali Pengo anasema kwamba, viongozi wa dini wanaowajibu mkubwa katika kuhimiza maadili, utii wa sheria na upunguzaji wa matukio ya uhalifu nchini Tanzania pamoja na kuhakikisha kwamba, Serikali inatekeleza wajibu wake msingi wa ulinzi na usalama kwa raia wake.

Viongozi wa Kanisa wanaweza kusaidia mchakato wa kuboresho ya maadili miongoni mwa jamii kwa njia ya mahubiri na mifano bora ya maisha, jambo ambalo linaweza kuwa ni msaada mkubwa katika kukabiliana na uhalifu ndani ya Jamii.

Mkuu wa Jeshi la Polisi kwa upande wake, amesema, umefika wakati kwa Jeshi la Polisi na Viongozi wa Kanisa kushirikiana kwa karibu zaidi ili kuhakikisha kwamba, utawala wa sheria unatekelezwa na kuzingatiwa na kwamba, wavunjaji wa sheria wanafikishwa mbele ya sheria. Ongezeko la vitendo vya uhalifu ndani ya Jamii ni changamoto kubwa hata kwa viongozi wa Kanisa, ambao wana wajibu wa kufundisha na kuhimiza maadili na utu wema.

Mkutano kati ya Kardinali Pengo na Mkuu wa Jeshi la Polisi umehudhuriwa pia na Askofu msaidizi Eusebius Nzigilwa pamoja na Askofu msaidizi Titus Mdoe wote kutoka Jimbo kuu la Dar es Salaam.







All the contents on this site are copyrighted ©.