Wakristo wanachangamotishwa kuishi na kushirikiana kwa pamoja kama kielelezo cha ushuhuda
wao kwa Kristo na Kanisa lake!
Baba Mtakatifu Francisko amemkaribisha Askofu mkuu Justin Welby wa Jimbo kuu la Cantebury
na Kiongozi mkuu wa Kanisa Anglikani duniani, kwa kutambua kwamba, Yeye si mgeni bali
ni sehemu ya "watakatifu na Familia ya Mungu". Anamshukuru kwa kumwombea wakati alipokuwa
anaanza utume wake kama Askofu wa Roma na kwamba, ni jambo jema kusindikizana kwa
njia ya sala.
Baba Mtakatifu amegusia historia tete ya uhusiano kati ya Kanisa
Katoliki na Kanisa Anglikani na jitihada ambazo Makanisa haya mawili imezitekeleza
katika kujenga na kudumisha upendo na udugu, jambo ambalo kwa pamoja wanapenda kumshukuru
Mungu.
Ni hija ambayo imeshuhudia kuundwa kwa Tume ya Ushirikiano wa Kimataifa
kati ya Makanisa haya mawili ili kuendeleza mchakato wa majadiliano ya kiekumene kwa
kuheshimiana na kuthaminiana katika kudumisha hali ya upendo na urafiki kama inavyojionesha
kwa uwepo wa Askofu mkuu Vincent Nichols Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Uingereza.
Baba
Mtakatifu Francisko anawashukuru viongozi wa Kanisa Anglikani kwa kutambua na kuthamini
mawazo na nia iliyopelekea Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita kuanzisha
Majimbo maalum ili kukidhi hamu ya Waamini wa Kanisa Anglikani waliotaka kwa hiyari
yao wenyewe kujiunga na Kanisa Katoliki. Ni matumaini ya Baba Mtakatifu Francisko
kwamba, waamini hao wataweza kushirikisha tasaufi, liturujia na mapokeo ya kichungaji
kutoka katika Kanisa Anglikani na hivyo kumwilisha amana hii kwa Kanisa Katoliki.
Mkutano
wa viongozi hawa wawili anasema Baba Mtakatifu Francisko ni kuwakumbusha kwamba, wanayo
dhamana ya kutafuta umoja miongoni mwa Wakristo kama sehemu ya utekelezaji wa utashi
wa Kristo mwenyewe aliyewaunganisha pamoja na kuwa kaka na dada na hivyo kuunda Familia
ya Baba mmoja na kwamba, sala yao ya pamoja ina umuhimu wa pekee katika hatima hii.
Sala inawawezesha Wakristo kuchuchumalia umoja unaopaswa kujionesha katika
medani mbali mbali za maisha, lakini zaidi kwa njia ya ushuhuda wa tunu msingi za
maisha ya Kikristo kama vile: utakatifu wa maisha ya mwanadamu; umuhimu wa familia
inayojengeka katika msingi wa uhusiano kati ya Bwana na Bibi wanaokamilishana; tunu
ambazo zinapewa kipaumbele cha pekee katika utume wa Askofu mkuu Welby.
Baba
Mtakatifu anasema kwa pamoja wanaweza kushirikiana kutafuta haki jamii, kujenga na
kudumisha uchumi ambao utatoa kipaumbele cha kwanza kwa binadamu na mahitaji yake
msingi, daima wakipania kutafuta mafao ya wengi na kuendelea kuwa ni sauti ya wanyonge
kama kielelezo cha upendo kwa Kristo aliyeonesha upendeleo wa pekee kwa binadamu,
lakini leo hii binadamu anaonekana kuwa kama mlaji asiye kuwa na thamani.
Baba
Mtakatifu Francisko anatambua kwamba, hizi ni kati ya changamoto ambazo Askofu mkuu
Welby anaendelea kuzipatia kipaumbele cha pekee katika utekelezaji wa utume wake sanjari
na kupania kuendeleza mchakato wa upatanisho na suluhu ya kinzani mbali mbali ndani
ya Jamii. Ni changamoto hii ambayo pia imetolewa na viongozi wa Makanisa nchini Uingereza
kuhakikisha kwamba, Jumuiya ya Kimataifa inasaidia upatikanaji wa suluhu ya mgogoro
wa kivita nchini Syria; kwa kuhakikisha kwamba, raia wanakuwa salama na uhuru wa kidini
unalindwa na kuheshimiwa.
Kama Wakristo wanapenda kushirikisha zawadi ya amani
na neema kwa ajili ya dunia, lakini zawadi hizi zinaweza kuzaaa matunda yanayokusudiwa
ikiwa tu Wakristo wataishi na kufanya kazi kwa ushirikiano na utulivu na hivyo kuchangia
katika hali ya kuheshimiana, amani na utulivu miongoni mwa waamini wa dini na imani
tofauti.
Baba Mtakatifu anahitimisha hotuba yake kwa kusema kwamba, umoja
wa Wakristo unaotafutwa unafumbatwa katika Fumbo la Utatu Mtakatifu na kwamba, wanapokutana
kama Wakristo watambue kwamba, Kristo yuko kati yao! Huu ni mwaliko wa kufanya hija
ya umoja wa Wakristo na udugu ambao unajikita katika upendo unaofanya rejea yake kwa
Kristo, ambaye ni maana ya hija hii katika maisha na utume wao!